Tuesday, August 19, 2014

KATIBU MKUU WA WIZARA YA UJENZI ARIDHISHWA NA UKARABATI WA KIVUKO CHA MV KIGAMBONI.


Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi Mhandisi Mussa Iyombe wapili kutoka kulia akipita kukagua matengenezo yanayoendelea ya Kivuko cha MV Kigamboni. Kulia kwake mwenye kofia ya njano ni Dkt. Wiliam Nsahama Mkurugenzi wa Huduma za Ufundi (DTES) kutoka Wizara ya Ujenzi

Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi Mhandisi Mussa Iyombe akiwa pamoja na viongozi wengine kutoka Wizarani na TEMESA wakiwa chini ya Kivuko cha MV Kigamboni kwa ajili ya Ukaguzi baada ya Matengenezo ya sehemu cha Chini.

Brigedia Jenarali Rogastian Shaban Laswai akitoa ufafanuzi kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi Mhandisi Mussa Iyombe kuhusiana na maendeleo ya ukarabati wa Kivuko cha Mv Kigamboni. Wa pili kulia ni Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) Mhandisi Marceline Magesa.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi Mhandisi Mussa Iyombe akiangalia maendeleo ya ukarabati wa Kivuko cha MV Kigamboni.


Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi Mhandisi Musa Iyombe ameelezea kuridhishwa kwake na kazi ya ukarabati wa Kivuko cha MV Kigamboni unaoendelea chini ya kikosi cha Ufundi cha Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), Kitengo cha Wanamaji uliofikia asilimia 40 ya matengenezo yake.

Akizungumza mara baada ya Ukaguzi huo wa kushtukiza, Mhandisi Iyombe amekipongeza Kikosi hicho cha Wanamaji kwa kufanya kazi kwa kiwango cha juu na haraka hivyo kuwa na matumaini ya kukamilika kwa kazi hiyo kwa muda mfupi ili kuondoa msongamano unaowakabili wananchi kwa sasa.

“Nia ya Serikali ni kuhakikisha kuwa Kivuko hiki kinakuwa katika ubora unaokubalika ili kulinda usalama wa abiria na mali katika huduma ya usafiri huu wa kila siku na unaotegemewa na wakazi wengi wa Kigamboni na maeneo jirani” Alisema Katibu Mkuu Mhandisi Iyombe.

Aidha, Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi amewaomba wananchi kuwa wavumilivu katika kipindi hiki kifupi cha ukarabati na kuahidi kuwa mnamo Septemba 7, Kivuko hicho kitaanza kazi zake kama kawaida.

“Kutokana na ukarabati unavyoendelea ni matumaini yangu kuwa kazi hii itakamilika kwa muda mlionieleza na itakuwa ya kiwango cha juu”. Katibu Mkuu alisema.
Mhandisi Iyombe aliahidi kutembelea tena katika Kivuko hicho mnamo mwanzoni mwa mwezi Septemba mara baada ya kukamilika kwake.
Kwa upande wa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), Mhandisi Marceline Magessa amesema kuwa hadi sasa ukarabati wa MV. Kigamboni upo katika hatua za marekebisho mbalimbali ikwemo utoaji kutu, kupaka rangi, usafi na uzibajji wa matundu pembezoni mwa kivuko hicho.

Nae Mkuu wa Jeshi la Wanamaji Tanzania Brigedia Jenerali Rogastian Shaban Laswai amafafanua ingawa kuna cha changamoto ya kina cha maji kinachokwamisha matengenezo ya Kivuko hicho bado wanaamini na wanajipanga kufanya kazi usiku na mchana kuhakikisha kwamba Septemba 7 kivuko hicho kitashushwa kwenye maji.

Ukarabati wa Kivuko cha MV Kigamboni chenye uwezo wa kubeba tani 160 na abiria 800 kwa wakati mmoja ulianza Agosti 14 mwaka huu.

0 Responses to “KATIBU MKUU WA WIZARA YA UJENZI ARIDHISHWA NA UKARABATI WA KIVUKO CHA MV KIGAMBONI.”

Post a Comment

More to Read