Tuesday, April 8, 2014

ALIYEKUWA AKIISHI KWENYE HANDAKI JIRANI NA MLIMANI CITY AONDOLEWA NA ASKARI, HANDAKI LACHOMWA MOTO.




CHACHA Makenge (38) aliyeripotiwa awali kuishi ndani ya handaki katika eneo la pori la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam sehemu ya Mlimani, amepatwa na balaa jipya baada ya makazi yake kuvamiwa na askari, kukamatwa na mwishowe kupelekwa Muhimbili kitengo cha wagonjwa wa akili kwa ajili ya matibabu.

Kana kwamba haitoshi, Makenge ambaye aliwahi kuishi katika handaki hilo kwa muda wa miaka mitano, alipotoka, alikuta makazi yake hayo yakiwa yamechomwa moto na vitu vyake vyote kuchukuliwa.

Akizungumza na gazeti hili, kijana huyo alikiri kutokewa na mambo hayo na kulalamika kuwa kitendo alichofanyiwa, kimempotezea mwelekeo wa maisha yake kwani hana tena sehemu ya kwenda kwa kuwa hakujiandaa.

Alisema alipokamatwa alipelekwa Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa kudhaniwa kuwa ni mgonjwa wa akili, lakini alipingana na madai hayo, licha ya kuwa aliishi kwa siku 36 hospitalini hapo kabla ya kuruhusiwa kuondoka.

Mmoja wa maofisa wa ulinzi wanaolinda chuoni hapo, Mussa Nakuwa aliyeendesha oparesheni ya kumkamata kijana huyo, alisema vifaa vyake vyote vilipelekwa Ofisi ya Ustawi wa Jamii Wilaya ya Kinondoni kwa ajili ya kuhifadhiwa na anaweza kwenda kuvichukua wakati wowote.

Habari zingine kuhusiana na mtu huyo zinadai amechimba mahandaki mengine kadhaa ya siri ambayo anayatumia kwa ajili ya kulala.

0 Responses to “ALIYEKUWA AKIISHI KWENYE HANDAKI JIRANI NA MLIMANI CITY AONDOLEWA NA ASKARI, HANDAKI LACHOMWA MOTO.”

Post a Comment

More to Read