Friday, April 11, 2014

ASKARI 10 WA USALAMA BARABARANI WAFUKUZWA KAZI.




JESHI la Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani limewafukuza kazi askari wake 10 kwa kosa la kwenda kinyume cha kanuni na  sheria za jeshi hilo.

Akizungumza na waandishi wa habari  jijini Dar es Salaam jana, Kamanda wa Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani nchini, Mohamed Mpinga, alisema  kuwa askari hao walipatikana na hatia baada ya kufunguliwa mashitaka ya kijeshi.

Alisema: “Baada ya kufunguliwa mashtaka yaliyokuwa yakiwakabili ya kwenda kinyume na mwenendo wa Jeshi la Polisi, walipatikana na hatia hivyo wengine tuliwafukuza na wengine kuwabadilisha vituo vyao vya kazi.”

Mpinga alisema wameamua kuwashughulikia askari hao ili kurejesha imani kwa wananchi ambao baadhi yao wameanza kupoteza imani wakiamini kuwa wapo askari wa barabarani wanaokiuka maadili ya jeshi hilo, lakini wanalindwa.

Ingawa Kamanda Mpinga hakutaja makosa ya askari hao, lakini habari za kipolisi kutoka ndani ya jeshi hilo wanadaiwa kuwa walijihusisha na vitendo vya rushwa, kinyume cha maadili na sheria za jeshi hilo.

“Hali hiyo imechangia kwa kiasi kikubwa utendaji wa kazi kuwa mgumu na jamii kutoamini kazi zinazofanywa na jeshi hilo, ndiyo maana tumeamua kuchukua hatua kali na tutaendelea kufanya hivyo kwa wengine wenye tabia hiyo,” alisema Mpinga.

Askari hao wamefukuzwa ikiwa ni siku chache baada ya Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam kutangaza kuwafukuza kazi askari wake wanne kwa makosa ya utovu wa nidhamu, ikiwemo kujihusisha na vitendo vya ujambazi.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam,  Suleiman  Kova, askari hao wanadaiwa kushiriki kwenye tukio la ujambazi lililotokea Machi 9, mwaka huu, eneo la Mbezi Beach baada ya kuvamia ofisi za Kampuni ya Kichina ya Hong Yang inayojishughulisha na kazi za ujenzi.

>>>via tanzania daima

0 Responses to “ASKARI 10 WA USALAMA BARABARANI WAFUKUZWA KAZI.”

Post a Comment

More to Read