Tuesday, July 15, 2014

APANDISHWA KIZIMBANI KWA KUJERUHI NA KUMTEMBEZA UCHI MWENZAKE MBELE ZA WATU



ZAITUNI Ally (30) mkazi wa manispaa ya Morogoro amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu mkazi mkoa wa Morogoro kwa tuhuma za kujeruhi na kumdhalilisha mwanamke mwenzie kwa kumtembeza mtupu mbele za watu.

Akisoma maelezo ya shitaka hilo, Mwendesha Mashtaka wa Polisi, Aminata Mazengo alidai mbele ya Hakimu Nuruprudensia Nassari kwamba mtuhumiwa huyo alitenda makosa mchana wa Julai 5 mwaka huu eneo la Msamvu B.

Ilidaiwa kwamba bila halali na akijua kufanya hivyo ni kosa kisheria, mshtakiwa alimkata Rehema Juma na kitu chenye ncha kali sehemu mbalimbali za mwili wake na kumsababishia maumivu.

Mwendesha mashataka huyo aliendelea kudai mahakamani hapo kwamba siku hiyo hiyo mtuhumiwa alimdhalilisha majeruhi huyo kwa kumlazimisha kutembea mtupu mbele za watu.

Hata hivyo, mtuhumiwa alikana makosa hayo na yupo nje kwa dhamana hadi kesi hiyo itakapotajwa tena Julai 24 mwaka huu kwa kuwa upelelezi haujakamilika.

0 Responses to “APANDISHWA KIZIMBANI KWA KUJERUHI NA KUMTEMBEZA UCHI MWENZAKE MBELE ZA WATU ”

Post a Comment

More to Read