Friday, August 1, 2014

WATENGENEZAJI WA FILAMU HIZI WACHUKULIWA HATUA NA BODI YA FILAMU TANZANIA.


Katibu Mtendaji Bodi ya Filamu Tanzania, Bi. Joyce Fissoo akiwaonyesha wahusika wa Kampuni za Jemedari Entertainment na Tanzania Commedian Unit (TCU) (hawapo pichani) baadhi ya vifungu vya Sheria vilivyokiukwa na wahusika hao.

Mmiliki wa Kampuni ya Jemedari Entertainment Bw. Mpole Gwatwambililege (kulia) akijitetea mbele ya Katibu Mtendaji wa Bodi ya Filamu kwa kutoa maelezo kuhusu kusambazwa kwa filamu hizo. Kushoto ni Katibu Mtendaji Bodi ya Filamu Tanzania, Bi. Joyce Fissoo na katikati ni Afisa Utamaduni Mkuu, Bi. Tabu Magembe na anayemfuatia ni Mwakilishi toka Kampuni ya Tanzania Commedian Unit (TCU) Bw. Geofrey Shaaban.Picha Zote Na Benedict Liwenga


Na Benedict Liwenga.

Bodi ya Filamu, katika ukaguzi wake wa kawaida uliofanyika tarehe 13 na 14 mwezi Machi, 2014, dhidi ya filamu zinazoingizwa sokoni bila kufuta utaratibu, imeweza kukamata filamu ambazo zilikuwa zimeingizwa sokoni bila kufuata taratibu, ikiwemo kukaguliwa na Bodi ya Filamu, kuwekewa madaraja na kupewa vibali.

Filamu zilizogundulika zikiwa sokoni ni Baunsa Kinyambe, Kanga Moko, Laki si Pesa, Muuza Genge na Mche wa Sabuni ambapo Bodi ilichukua hatua ya kuwatafuta wahusika, na kupitia matangazo ya filamu hizo walielekezwa kuziwasilisha kwa ukaguzi pamoja na kuacha kuendelea kuzisambaza hadi zitakapokaguliwa na kupewa vibali.

Kukamatwa kwa filamu hizo kunatokana na ukaidi wa wahusika kutowasilisha kazi zao kama walivyoelekezwa hapo awali licha ya kutumiwa ujumbe kwa njia ya simu.

“Tarehe 15/04/2014, wahusika tuliwatumia ujumbe kwa njia ya simu ili kuwakumbushia kuziwasilisha kazi zao lakini hawakujibu ujumbe huo na baada ya jitihada mbali mbali za kuwatafuta, wahusika hawa waliziwasilisha tarehe 31/07/2014”. Alisema Bi. Fissoo

Akizungumzia waliowasilisha kazi zao katika Bodi ya Filamu ni Jemedari Entertainment, ikiwakilishwa na Mpole Gwatwambililege ambaye ndiye mmiliki wa Kampuni hiyo pamoja na Bwana Geofrey Shaaban aliyeiwakilisha Tanzania Commedian Unit.

Wahusika hawa walitoa ufafanuzi ufuatao kwa Bodi ya Filamu kuhusu uwepo wa filamu hizo na kutokukaguliwa kwake huku zikiwa zimeshasambazwa na kwa upande wake Mmiliki wa Jemedari Entertainment, Bwana Mpole Gwatwambililege aliieleza Bodi kuwa mwanzoni mwa mwezi Machi 2014 alipigiwa simu na Bodi ya Filamu ikimtaka awasilishe filamu tajwa kwa ukaguzi huku akisema kuwa kwa wakati huo alipopigiwa simu alikuwa safarini nje ya Dar es Salaam na alirudi Dar es Salaam mwezi Julai 2014 na alipofika Dar es Salaam aliwasili Bodi ya Filamu na kuelekezwa kuwasilisha filamu husika kama alivyotakiwa na Bodi.

“Ilinilazimu kwenda sokoni kuzitafuta filamu hizo na kufanikiwa kuzipata ingawa kwa maelezo niliyoyapata kutoka sokoni nilielezwa kuwa msambazaji wa filamu hizo tano ni wale wale wasambazaji niliowapa kazi ya kunisambazia filamu ya Mr. Damian ambayo niliitengeneza awali iliyopewa kibali Na. 0003450 na Wasambazaji hao ni Tanzania Comedian Unit”.Alisema Gwatwambililege.

Bwana Gwatwambililege aliongeza kuwa ilimlazimu kuwatafuta vijana waliozisambaza filamu hizo tano na kuwahoji ambapo wao walimueleza kuwa aliyewaelekeza kusambaza filamu hizo ni Bwana Duncan Simon na kwa maelekezo ya Bwana Duncan Simon, wakatengeneza filamu tano ambazo ni Baunsa Kinyambe, Kanga Moko, Laki si Pesa, Muuza Genge na Mche wa Sabuni.

Kwa mujibu wa taarifa ya Kikao kilichofanyika kati ya Bodi ya Filamu na wahusika taarifa inaeleza kwamba, kabla ya safari, Bwana Mpole Gwatwambililege aliwapa Tanzania Commedian Unit kazi ya kuisambaza filamu ya Baunsa Kinyambe huku akiwa amewaelekeza kuiwasilisha Bodi ya Filamu kwa Ukaguzi kwanza. Wahusika aliowapa kazi ya kuisambaza hawakuiwasilisha Bodi kwa Ukaguzi na wala hawakuisambaza filamu hiyo kwa taratibu walizoelekezwa bali walinakili baadhi ya vipande vyake na kuichanganya na Filamu za Muuza Genge na Mche wa Sabuni. Baada ya hapo walitengeneza filamu nyingine mbili, yaani Kanga Moko na Laki si Pesa na kuziingiza zote sokoni.

Kwa upande wao Tanzania Commedian Unit ambayo iliwakilishwa na Geofrey Shaaban walikili wakisema kuwa maelezo yaliyotolewa na Jemedari Entertainment yapo sahihi na hawahitaji kuongeza au kukana kitu chochote.

Katika kikao hiko Bi. Fissoo alifafanua kuwa, Tasnia ya Filamu inasimamiwa na Sheria ya Filamu na Michezo ya Kuigiza Na. 4 ya 1976 na Kanuni zake Na. 156 za mwaka 2011. Hivyo, wahusika wanatakiwa kufahamu kuwa kuingiza filamu sokoni bila kufuata taratibu ni kosa kwa mujibu wa Sheria tajwa na Kanuni zake.

“Kikao kimepitishwa katika vifungu mbali mbali vya Sheria na Kanuni zinazoelekeza hatua zinazopaswa kufuatwa na hatua zinazochukuliwa dhidi ya wale wasiofuata taratibu, vifungu hivi vya Sheria ni Kifungu cha 3 hadi cha 6 kikisomwa pamoja na kifungu cha 4 cha Kanuni za Sheria hiyo, vifungu vya 14 hadi 18 vya Sheria kuhusu ukaguzi wa filamu vikisomwa pamoja na kifungu vya 25 mpaka 27 na kifungu cha 47 (1 na 2 A mpaka C vya Kanuni za Sheria ya Filamu na Michezo ya Kuigiza. Aidha, Tanzania Comedian Unit, walijulishwa bayana kuhusu kughushi alama ya ukaguzi ya kazi nyingine na kuiweka katika kazi tofauti suala ambalo litapeleka kwenye kikao cha Bodi kitakachofuata”.Alisisitiza Bi. Fissoo.

Filamu za Kanga Moko na Laki si Pesa zilishapigwa marufuku. Kuendelea kuwepo sokoni ni kukiuka Sheria, Kanuni na Taratibu na pia utengenezaji na uingizaji filamu sokoni bila kufuata taratibu ni kosa na kwa mujibu wa kifungu cha 47 (a 1 na 2 na b. 1) cha Kanuni za Sheria ya Filamu na Michezo ya Kuigiza ya 1976, ambapo vimeipa Bodi Mamlaka ya kuamuru kusitisha filamu hizo. Hivyo, Kifungu cha 32 kimeipa Bodi ya Filamu mamlaka ya kuikubali au kuikataa filamu yoyote baada ya kuikagua. Kwa mujibu wa kifungu cha 47, 1 na 2 wahusika wametakiwa kulipa faini ya papo kwa papo ya shilingi milioni moja kwa kila kampuni kama ilivyofafanuliwa katika vifungu vya Sheria.

Aidha, Filamu za Baunsa Kinyambe, Muuza Genge na Mche wa Sabuni zitapitiwa na kutolewa maamuzi na Bodi ya Filamu hivyo haziruhusiwi kwenda sokoni mpaka zitakapokaguliwa na kupewa kibali. Bodi imewataka wahusika pia watafute muda wao kwa kutumia vyombo vya habari wawaombe radhi watanzania kwa kuwapelekea kazi tukanishi na Nakala hiyo ya kuomba radhi iwasilishwe Bodi ya Filamu.

0 Responses to “ WATENGENEZAJI WA FILAMU HIZI WACHUKULIWA HATUA NA BODI YA FILAMU TANZANIA.”

Post a Comment

More to Read