Monday, February 23, 2015
JESHI LA KUJENGA TAIFA (JKT) WATOA KAULI KUHUSU WAHITIMU WAO KUANDAMANA
Do you like this story?
JESHI la Kujenga Taifa (JKT) limewataka
vijana waliomaliza katika jeshi hilo, kutambua kuwa walikula kiapo cha utii
wakati wa kuhitimu mafunzo, hivyo suala la kuandamana ni kinyume na kiapo chao.
Vijana hao waliotumikia Jeshi la
Kujenga Taifa Operesheni za nyuma na kumaliza mkataba wa miaka miwili,
wameambiwa shinikizo lao la kulazimisha ajira kwa kuandamana ni kinyume cha
sheria za nchi.
Taarifa kwa vyombo vya habari
iliyotolewa na Makao Makuu ya jeshi hilo, jijini Dar es Salaam mwishoni mwa
wiki, ilisema kipengele kimoja cha masharti ya kujiunga na JKT kinasema baada
ya mkataba, wanapaswa kurejea nyumbani na hawapaswi kudai jeshi liwatafutie
ajira. Ilieleza kwamba masharti ya jeshi hilo, huwekwa bayana kwa vijana
wanapojiunga na JKT.
Vijana hao wanatakiwa kujua masharti
hayo na taratibu za JKT na kuelewa kuwa JKT halitoi ajira. Taarifa hiyo
ilinukuu kipengele kimojawapo cha masharti, kinachosema “Kwa kipindi chote
nitakachokuwa ndani ya Jeshi la Kujenga Taifa nitakuwa nafanya mafunzo ya
kijeshi na ya stadi za kazi na maisha, na baada ya mkataba nitarejea nyumbani.
Hivyo sitalidai Jeshi la Kujenga Taifa ajira, wala kulitaka linitafutie ajira/
kazi”.
Ufafanuzi huo ulitolewa, kutokana na
vijana zaidi ya 200 waliohitimu mafunzo ya JKT kuanzia mwaka 2000 hadi mwaka
2013, kutangaza wiki iliyopita kuwa wataandamana siku yoyote wiki hii kwenda
kwa Rais Jakaya Kikwete, kumweleza shida zao, ikiwemo kutokuwa na ajira tangu
wamalize mafunzo.
Jeshi hilo lilisema ni vema vijana hao,
wakatambua kuwa tatizo la ajira siyo kwao peke yao, ni tatizo la ulimwengu
mzima Tanzania, ikiwemo hivyo wanashauriwa kutumia stadi za kazi kujiajiri
wenyewe.
“Kutokana na dhumuni la kuundwa JKT
Taifa, halina dhamana ya kuajiri bali kufunza vijana wa taifa hili umoja, stadi
za kazi na uzalendo baada ya hapo wawe wenye sifa za kuajiriwa hupata ajira
katika taasisi mbalimbali za serikali na binafsi,” ilisema taarifa hiyo.
Hata hivyo, jeshi hilo limesema tangu
mwaka 2003 hadi 2014, vijana 24,708 wameajiriwa katika vyombo vya ulinzi na
usalama. Kati ya hao, vijana 21,977 wakiwemo wavulana 17,307 na wasichana
4,670, wameajiriwa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).
Kwa upande wa Polisi, vijana 3,965
wameajiriwa ambao kati yao, wavulana ni 2,943, Magereza wameajiriwa 2,139 kati
yao wavulana ni 2,044, Zimamoto vijana 100 wavulana wakiwa 78 na taasisi
zingine wameajiriwa vijana 592.
Aidha, vijana 1,622 wameajiriwa katika
taasisi mbalimbali kama vile migodi ya dhahabu ya Geita, Mamlaka ya Bandari
Tanzania (TPA) na Shirika la Hifadhi za Taifa (Tanapa).
Taarifa hiyo ilisema JKT ilianzishwa
Julai 10, 1963 kwa lengo la kuwaweka pamoja vijana na kuwapa malezi, kuhusu
uzalendo na umoja ili kuondoa dalili za matabaka, zilizoanza kujitokeza katika
jamii baada ya uhuru.
Serikali ilirejesha mafunzo ya jeshi
hilo kwa vijana wa kujitolea mwaka 2001 baada ya kusitishwa mwaka 1994.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “JESHI LA KUJENGA TAIFA (JKT) WATOA KAULI KUHUSU WAHITIMU WAO KUANDAMANA ”
Post a Comment