Monday, February 23, 2015
NJOMBE IWE MFANO BORA WA DAFTARI LA WAPIGAKURA.
Do you like this story?
LEO Tanzania inaanza kutekeleza hatua
muhimu ya kutimiza matukio mazito, yanayosubiriwa kwa hamu mwaka huu na
Watanzania nchi nzima ya upigaji kura ya maoni katika Katiba Pendekezwa na
uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba, mwaka huu.
Hatua hiyo muhimu ni kuanza rasmi
kujiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapigakura kupitia mfumo mpya wa
Biometric Voters Registration (BVR), ambao unaanza leo mkoani Njombe.
Tayari Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC)
ilishaufanyia majaribio mfumo huo katika baadhi ya maeneo ndani ya mikoa mitatu
ya Dar es Salaam, Morogoro na mkoani Katavi.
Kwa mujibu wa taarifa ya tume, pamoja
na changamoto chache zilizobainika, katika maeneo hayo tume ilifanikiwa kwa
asilimia kubwa na ina uhakika mfumo huo utatumika kuwaandikisha Watanzania wote
katika daftari hilo bila matatizo.
Tume hiyo ilitaja changamoto chache
zilizojitokeza katika majaribio hayo kuwa ni mfumo mzima wa BVR ulivyoandaliwa
(setting), hardware na programu zinazotumiwa na mfumo huo na maeneo ya
uendeshaji uandikishaji huo.
Tume hiyo imewahakikishia Watanzania kuwa
changamoto zote hizo, zimefanyiwa kazi kwa kurekebishwa, ambapo pia BVR
zitakazotumika mkoani Njombe, nazo zimefanyiwa marekebisho kutokana na
changamoto zilizojitokeza.
Kutokana na maandalizi hayo ni wazi
kuwa sasa utaratibu mzima wa watu kujiandikisha katika daftari la kudumu,
unaanza rasmi mkoani Njombe.
Hivyo, ni vyema wakazi hao wakajitokeza
kwa wingi na kutumia haki yao ya kujiandikisha ili waweze kushiriki vyema
katika matukio mawili makubwa ya uchaguzi.
Hapa nchini katika chaguzi nyingi zilizopita,
ilizoeleka kuona idadi ndogo ya watu wenye umri wa kupiga kura kujitokeza
kupiga kura, jambo linalosababisha hata ushiriki katika uchaguzi na wale
wanaojitokeza kupiga kura pia uwe mdogo.
Ikumbukwe kuwa kila mtu aliyetimiza
miaka 18 ana haki ya kujiandikisha katika daftari hilo na kushiriki kikamilifu
katika uchaguzi wa kura ya maoni kupigia kura Katiba Pendekezwa na pia
kushiriki katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu, kuchagua viongozi watakaoliongoza
taifa.
Hivyo basi ni vyema wakazi wa Njombe, wakawa
mfano mzuri kwa watanzania wa mikoa mingine inayosubiri utaratibu huo wa
kujiandikisha, kwa kujitokeza kwa wingi kujiandikisha ili ratiba ya
uandikishaji itakavyosogea katika mikoa mingine, watu wawe na mwamko wa
kushiriki kikamilifu.
Wapo baadhi ya watu kazi yao ni
kulalamika, kunyoosha vidole na kuishia kufanya vurugu matukio muhimu kama hayo
yanapojitokeza.
Watu kama hao badala ya kujitokeza na
kushiriki, hutafuta visingizio na baadaye wanapokosa fursa ya kushiriki katika
uchaguzi huwa wa kwanza kuanzisha vurugu. Tutambue kuwa kila Mtanzania ana haki
ya kupiga kura pale atakapofikisha umri wa miaka 18.
Ikumbukwe pia kuwa mtu hawezi kushiriki
katika uchaguzi huo na kumchagua kiongozi anayemtaka, kama hatajiandikisha
katika daftari hilo la wapiga kura.
Hivyo basi, wakazi wa Njombe watambue
kuwa macho na masikio ya watanzania wote kuanzia leo yapo mkoani humo,
wakifuatilia kwa kina utaratibu mzima wa kujiandikisha katika daftari hilo,
hasa kupitia mfumo huo wa BVR, ambao umezua gumzo nchini tangu utambulishwe na
NEC.
Kutokana na ukweli huo, ni wajibu kwa
wakazi wa Njombe kushiriki kikamilifu katika shughuli hiyo.
Pia, tume yenyewe ni lazima ihakikishe
kuwa ahadi iliyotoa kwa watanzania, kupitia matokeo ya majaribio ya
uandikishaji wananchi kupitia mfumo huo wa BVR, inatekelezeka na uandikishaji
huo mkoani Njombe unafanyika kwa mafanikio.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “NJOMBE IWE MFANO BORA WA DAFTARI LA WAPIGAKURA.”
Post a Comment