Tuesday, October 13, 2015
TUME YA TAIFA YA UCHAGUZI(NEC) YAFYEKA WAPIGA KURA MILIONI MOJA,WALIOJIANDIKISHA WALIKUWA 23,782,558.
Do you like this story?
Tume ya Taifa
ya Uchaguzi (NEC), imeyaondoa majina ya wapiga kura zaidi ya milioni moja
kutoka katika orodha ya awali ya watu milioni 23.7 waliojiandikisha awali
kwenye Daftari la Kudumu la Wapigakura kwa mfumo wa kielektroniki (BVR).
Akizungumza
kwenye mkutano wa NEC na viongozi wa vyama vya siasa jijini Dar es Salaam jana,
Mwenyekiti wa NEC, Jaji mstaafu Damian Lubuva, alisema hatua ya kupunguzwa kwa
idadi ya wapiga kura inatokana na kukamilika kwa kazi ya uhakiki wa majina ya
watu wote waliojiandikisha.
Alisema kuwa
awali, idadi ya watu walioandikishwa kupiga kura ilikuwa 23,782,558.
Hata hivyo,
baada ya uhakiki, imebainika kuwa majina 1,031,769 kutoka miongoni mwa orodha
ya awali hawastahili kuwamo kwani baadhi yao ni majina ya watu waliojiandikisha
zaidi ya mara moja, wengine siyo Watanzania na wapo pia waliokosa sifa nyingine
muhimu za kupiga kura, kwa mujibu wa sheria za nchi.
Kwa sababu
hiyo, Jaji Lubuva alisema idadi halisi ya watu watakaokuwa na fursa ya kupiga
kura Oktoba 25 ni 22,251,292 kwa Tanzania Bara na wengine 503,193 wa visiwani
Zanzibar.
Jaji Lubuva
alieleza zaidi kuwa baada ya uhakiki na uchakataji wa taarifa za wapiga kura,
NEC ilibaini kuwa wananchi 181,452 walijiandikisha zaidi ya mara moja, huku
baadhi yao wakitia fora kwa kujiandikisha hadi mara nane.
Akifafanua
zaidi, mwenyekiti huyo wa NEC alisema uhakiki umebaini kuwa wananchi 845,944
waliandikishwa na waandishaji 74,502 waliokuwa kwenye mafunzo ya vitendo kabla
ya kuanza uandikishaji, hivyo majina yao yameondolewa, huku majina 3,870
yakibainika kuwa ni ya watu wasiokuwa raia wa Tanzania na hivyo, taarifa zao
pia zimefutwa.
VITUO VYA KURA
VYAPANGULIWA
Katika hatua
nyingine, NEC imetangaza idadi rasmi ya vituo vya kupigia kura nchini kuwa ni
65,105, kati yake 1,580 vikiwa visiwani Zanzibar na vilivyobaki (63,525) vikiwa
Tanzania Bara. Idadi hii ni pungufu kulinganisha na idadi ya vituo
vilivyokadiriwa awali kabla ya kufanyika kwa uhakiki, ambavyo NEC ilitangaza
kuwa vitakuwa 72,000 na kwamba, vinaweza kuongezwa au kupunguzwa kulingana na
mahitaji kadiri itakavyoonekana inafaa. Kadhalika, idadi hiyo iliibua shaka pia
kutoka kwa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) vya Chadema,
CUF, NCCR-Mageuzi na NLD.
Mgombea mwenza
wa Ukawa, Juma Duni Haji, alielezea shaka waliyonayo wiki iliyopita kwa kudai
kuwa wastani wa wapiga kura 450 kwa kila kituo unahitaji vituo takribani 53,000
tu kuhudumia wapiga kura milioni 23.7 na siyo 72,000. Duni aliongeza kuwa Ukawa
wanahofia kuwapo kwa njama za kukibeba Chama Cha Mapinduzi (CCM) kupitia vituo
bandia 20,000 vilivyoongezeka kulingana na mahitaji na uwezo wa kila
kituo.
Hata hivyo, NEC
ilipuuza madai hayo kwa kueleza kuwa hakuna vituo vyovyote bandia na kwamba
idadi hiyo ni ya makadirio ya awali kabla ya uhakiki.
Katika hotuba
yake ya ufunguzi wa mkutano wa jana, Jaji Lubuva alisema kila kituo kinapaswa
kuwa na idadi ya wapiga kura kati ya 450 hadi 500, na kwamba ikitokea kuna
kituo kinakuwa na wapiga kura zaidi ya 500, watakachofanya ni kukigawanya katika
vituo viwili vyenye idadi sawa ya wapiga kura.
“Hiyo ndiyo
idadi ya vituo vitakavyotumika siku ya uchaguzi. Isipokuwa wananchi wanapaswa
kuhakiki taarifa zao siku nane kabla ya uchaguzi ili kujiepusha na usumbufu
utakaotokana na mgawanyo wa vituo,” alisema.
MAJIMBO,
KATA
Lubuva alisema
NEC imetekeleza wajibu wake wa kuongeza majimbo mapya 25 na pia Ofisi ya Waziri
Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) imeanzisha kata mpya 622,
hivyo jumla ya majimbo yatakayogombewa kwa nafasi za ubunge ni 264 na kata zote
ni 3,957.
Aliongeza kuwa
uchaguzi wa wabunge katika majimbo matatu umeahirishwa baada ya kutokea kwa
vifo vya wagombea. Majimbo hayo ni Ulanga Mashariki lililompoteza mgombea
kutoka CCM, Celina Kombani; Jimbo la Lushoto lililompoteza mgombea kutoka
Chadema, Mohamed Mtoi na Jimbo la Arusha Mjini lililoondokewa na mgombea ubunge
kutoka ACT-Wazalendo, Estomiah Mallah.
Aliongeza kuwa
uteuzi wa wagombea umeshafanyika katika majimbo ya Ulanga Mashariki na Lushoto
na kwamba jana na kwamba, kampeni zitaanza leo hadi Novemba18 huku uchaguzi wao
ukitarajiwa kufanyika Novemba 22. Ratiba ya uchaguzi wa Jimbo la Arusha mjini
bado haijatolewa.
MNYIKA AISHNGAA
NEC
Naibu Katibu
Mkuu wa Chadema (Bara), ambaye pia ni mgombea ubunge wa Jimbo la Kibamba, John
Mnyika, alisema chama chake kiliandika barua wakidai kuwa wapatiwe orodha ya
majina ya wapigakura pamoja na idadi ya vituo vya kupigia kura, lakini
anashangaa kuona kuwa hilo halikufanyika.
“Nashangaa
barua hiyo nimekabidhiwa leo, lakini haijaeleza ni lini orodha hiyo
itapatikana,” alisema.
Mgombea urais
wa Zanzibar kupitia Tadea, Juma Ali Khatibu, alielezea wasiwasi wao juu ya
kutegemea mawasiliano kwa njia ya mkongo wa taifa katika utoaji wa matokeo,
akisema kuwa kufanya hivyo ni sawa na kuchelewesha matokeo na kusababisha
usumbufu kwa wapigakura.
Mwenyekiti wa
ADC, Said Miraji, alisema kuwa changamoto iliyopo kwa NEC ni kutoaminika
kutokana na historia ya viongozi wao waliotangulia, hivyo aliwataka waliopo
kuacha tabia ya kulalamika na badala yake watatue matatizo yaliyopo.
Mgombea ubunge
wa Jimbo la Ubungo ambaye pia ni Katibu Mwenezi wa Chama cha Ukombozi wa Umma
(Chaumma), Kabendera Eugen, alisema hakuna sababu ya kuwa na hofu na NEC, bali chombo
hicho kinapaswa kufuata taratibu na haki.
Akijibu maswali
na hoja mbalimbali zilizoibuliwa na viongozi wa vyama, Mkurugenzi wa NEC,
Kailima Ramadhan, alisema kuwa baada ya kutangaza idadi ya wapigakura na vituo,
sasa kila kitu kimekamilika na kuwataka viongozi wa vyama vya siasa kuwasiliana
na NEC ili kupatiwa orodha hizo.
Pia, Kailima
aliwatoa hofu viongozi wa vyama vya siasa kwa kuwaleza kuwa mfumo watakaoutumia
kutoa matokeo umehakikiwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Maendeleo
(UNDP) kupitia wataalamu mbalimbali, baadhi wakitoka nchini Ufaransa.
“Kila kitu
kitafanyika kwa uwazi. Hivyo hakuna sababu ya kuwa na hofu... kila kitu
kitakuwa salama,” alisema
Aidha, alisema
uchaguzi ni kazi kubwa na muhimu na kuhusisha wadau wengi, vikiwamo vyama vya
siasa, hivyo mafanikio yanategemea ushirikiano mzuri wa NEC na vyama.
Alisema wao
wamejipanga kusimamia na kuhakikisha kuwa daima haki inatendeka ili kulinda
amani na utulivu na kwamba, kwa sababu hiyo, ni wajibu wa vyama vya siasa
kutumia majukwaa yao kuwaelimisha wafuasi wao kutokusanyika jirani na vituo vya
kura, bali watekeleze wajibu wao wa kupiga kura na kuondoka.
Mkutano wa jana
kati ya NEC na vyama vya siasa ulikuwa na lengo la kujadiliana na kubadilishana
mawazo kuhusu masuala mbalimbali ya Uchaguzi Mkuu na pia kupeana taarifa kuhusu
maandalizi ya uchaguzi.
CHANZO: NIPASHE
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “TUME YA TAIFA YA UCHAGUZI(NEC) YAFYEKA WAPIGA KURA MILIONI MOJA,WALIOJIANDIKISHA WALIKUWA 23,782,558.”
Post a Comment