Kumbilamoto ambaye pia ni Diwani wa kata ya Vingunguti kupitia Chama cha Wananchi (CUF) amesema kuwa chama hicho kilikuwa ni kimbilio la wananchi wanyonge lakini kwa sasa kimekuwa ni cha kilio kuanzia viongozi mpaka wanachama wenye mapenzi ya dhati.
“CUF inatia huzuni, Inahitaji maombi ili migogoro iishe, nawaonea huruma sana viongozi hasa madiwani ambao huu mgogoro unawaumiza kwa sababu ni siku chache tu zilizobaki kufikia uchaguzi mkuu wa 2020 kama hawajafanya kitu ni ngumu sana kuja kuwashawishi tena wananchi wawachague,”amesema Kumbilamoto.
Aidha, amesema kuwa mgogoro huo umekivuruga chama ambacho kilikuwa kimbilio la wengi lakini kwa sasa kimekuwa chama cha kulia lia na kutapa tapa sababu ya mgogoro ambao umekuwa ni sumu ndani ya chama hicho.
Vile vile amewaomba waandishi wa habari kusaidia kutatua mgogoro huo kwa kutumia kalamu zao pamoja na hekima zao kufikisha ujumbe kwa jamii na viongozi mbalimbali wa chama hicho.
Hata hivyo, mbali na hayo kiongozi huyo amesema hana mpango wa kuendele kung’ang’ania madarakani endapo pale umri wake wa kuwa kwenye siasa utakuwa umekwenda na kwamba atahitaji mapumziko kwani kiongozi mwenye nia ya kutumikia wananchi huwa haoni utamu wa uongozi.