Monday, April 7, 2014

MSEKWA:SITTA ANA LAKE JAMBO.




Siku moja baada ya Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samwel Sitta kukiri kuchezewa kwa saini ya aliyekuwa Katibu wa Bunge la Tanganyika, Pius Msekwa na Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, Msekwa amesema, ‘mzungumzaji huyo ana lake jambo’.

Sitta akizungumza na gazeti hili juzi mjini Dodoma alisema ni kweli kuna maneno katika hati hiyo ya sheria namba 22 ya 1964, iliyosainiwa na Nyerere na Msekwa, Aprili 25, 1964, yameongezwa.

Alifafanua kuwa saini ya Nyerere imeongezwa herufi ‘us’ kwa kompyuta na katika sehemu ya saini ya Msekwa kumeandikwa neno ‘Msekwa’ kwa kompyuta, jambo ambalo ni makosa. Sitta alisema walioongeza maneno hayo ni wafanyakazi wa ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali baada ya kuona sehemu ya maandishi kwenye saini hizo hayasomeki, lakini walifanya makosa.

Msekwa akizungumza na gazeti hili jana alisema: “Saini iliyo katika hati original (halisi) ni ya kwangu mimi, lakini huyo anayesema zimechezewa muulizeni atakuwa na lake jambo. Kama kompyuta imekosea ni leo kwa kuwa kipindi hicho kompyuta hazikuwapo.”
Aliongeza: “Ana lengo gani la kutilia shaka, ana lengo gani la kusema imechakachuliwa, kinachotakiwa ni hati original ambayo iko ofisi ya Katibu wa Bunge itolewe, kwanini tuendelee kuandikia mate wakati wino upo?”

Mjumbe wa Bodi ya Kituo cha Taarifa kwa Wananchi Umma (TCIB), Hebron Mwakagenda alisema yote hayo yanatokea ni kuvuruga hoja iliyopo mezani.

Alisema kitendo cha kupoteza muda kuzungumzia suala la kuchezewa kwa saini halitakiwi kwani kama maudhui yake hayakuchezewa basi hoja ya muundo wa Muungano uamuliwe na wananchi wenyewe.

“Tusianze kupoteza muda kwa mambo ambayo hayapo cha msingi wananchi wenyewe waulizwe wanaupenda Muungano au la lakini tusianze kumtafuta mchawi kuwa saini zimechezewa wananchi waamue wenyewe kuhusu Muungano,” alisema Mwakagenda.

0 Responses to “MSEKWA:SITTA ANA LAKE JAMBO.”

Post a Comment

More to Read