Thursday, May 15, 2014
SERIKALI INAFANYA MZAHA NA UGONJWA WA DENGUE
Do you like this story?
Waombolezaji wakibeba jeneza lenye mwili wa Daktari Gilbert Buberwa wa Hospitali ya Temeke kwa ajili ya kuagwa. Daktari huyo, aliyefariki kwa kuugua homa ya dengue. Picha na Rafael Lubava |
Nchi
nzima imekumbwa na taharuki kutokana na watu zaidi ya 400 kuugua homa ya dengue
na tayari watu watatu wamepoteza maisha, akiwamo daktari bingwa wa magonjwa ya
akili aliyekuwa akifanya kazi Hospitali ya Temeke, jijini Dar es Salaam. Hofu
hiyo kwa kiasi kikubwa imetokana na habari kwamba ugonjwa huo hauna tiba wala
chanjo na husababishwa na aina ya mbu ajulikanaye kama aedes, ambaye husambaza
maradhi hayo nyakati za mchana.
Kinachotia
hofu zaidi ni mwenendo usioridhisha wa Serikali ambayo imekuwa kama mtazamaji
katika kupambana na ugonjwa huo. Badala ya kuongoza na kuonyesha njia, kwa
maana ya kubuni mikakati ya kupunguza kasi ya ugonjwa huo na kutoa taarifa za
uhakika na kwa wakati kwa wananchi, Serikali imejenga taswira ya kutokuwa na
uwezo katika mapambano hayo. Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii ilisema juzi
kwamba itapeleka taarifa za kuwapo kwa ugonjwa huo nchini katika Shirika la
Afya Duniani (WHO) kama mwongozo wa kanuni za afya za kimataifa unavyoelekeza.
Kitu
muhimu hapa ni aina ya taarifa zitakazotumwa kwa shirika hilo, kwani
kulitaarifu tu kuhusu uwapo wa janga hilo hapa nchini siyo muhimu kwa kuwa
tayari suala hilo linajulikana.
Kinachotakiwa ni taarifa zenye takwimu sahihi,
ikiwa ni pamoja na idadi kamili ya watu walioambukizwa na maeneo wanakotoka.
Tunasema hivyo kutokana na takwimu zilizotolewa na Serikali kutiliwa shaka na
kukosa uhalisia kulingana na ukubwa wa tatizo.
Kwa mfano, inakadiriwa kwamba
idadi ya watu walioambukizwa ugonjwa huo ni kubwa mno kulinganisha na idadi ya
watu 400 nchi nzima iliyotajwa na Serikali juzi. Taarifa tulizonazo ni kwamba
Hospitali ya Mwananyamala pekee imepata wagonjwa wapatao 300 kati ya Aprili na
mwezi huu.
Ofisi
ya WHO iliyopo jijini Dar es Salaam jana ilitoa tahadhari kwamba dengue sasa ni
janga na kuonya kuwa, zisipopatikana takwimu sahihi za ugonjwa huo nchi nzima,
hali itakuwa mbaya sana baadaye. WHO ilisema ugonjwa huo ni suala mtambuka, kwa
maana ya kuzigusa wizara nyingine nyingi, hivyo isiachiwe Wizara ya Afya pekee,
bali pia wizara zinazohusika na miundombinu, maji, ujenzi na kadhalika lazima
zihusishwe.
WHO
inasema pia kwamba lazima utafiti ufanyike ili kujua tabia za mbu hao na virusi
vipi vimesambazwa kulinganisha na maeneo mengine yenye ugonjwa huo. Dengue
iliingia nchini mwaka 2010 na kuua baadhi ya wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa
Fedha (IFM). Serikali haikutaka kuufahamu ugonjwa huo na hivi sasa ndipo
taasisi zake kama Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi cha Muhimbili (MUHAS) na
Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMRI) zinahaha kufanya tafiti ili
kuufahamu na kuishauri Serikali.
Tunaitaka
Serikali ielekeze nguvu zake katika kuutokomeza ugonjwa huo. Zinahitajika fedha
nyingi, vifaa na vitendea kazi vya kuchukulia vipimo na kutoa kinga kwa wauguzi
na madaktari ili wasizidi kuambukizwa na kupoteza maisha. Vipimo visitozwe
fedha ili kunusuru maisha ya wagonjwa wasio na uwezo kifedha.
Ianzishwe
operesheni maalumu kunyunyizia dawa katika mazalio ya mbu na kazi hiyo iwe
endelevu badala ya zimamoto. Matarajio yetu ni kwamba Serikali haitafanya mzaha
tena katika kupambana na homa ya dengue.
Chanzo;Mwananchi
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “SERIKALI INAFANYA MZAHA NA UGONJWA WA DENGUE”
Post a Comment