Thursday, May 15, 2014
UDA ZINAZOKATIZA SAFARI DAWA IMEIVA
Do you like this story?
Mamlaka
ya Udhibiti wa Usafiri wa Vyombo vya Majini na Ardhini (Sumatra) imeliamuru
Shirika la Usafiri Dar es Salaam (Uda) kuandika maeneo ya safari kwenye mabasi
yake kutokana na madai ya kukatisha safari.
Akizungumza
na gazeti hili jana, meneja leseni wa Sumatra, Leo Ngowi alisema wamelazimika
kutoa amri hiyo baada ya kupokea malalamiko ya usumbufu na gharama wanazopata
abiria wanaotumia usafiri wa mabasi hayo sehemu mbalimbali za jiji.
“Nimezungumza
na mmoja wa maofisa wa Uda na tumekubaliana kuanzia leo waanze kutekeleza
utaratibu huo,” alisema na kuongeza:
“Tusingependa
kusikia tena abiria wanapata mateso na usumbufu usio na ulazima kwa kutumia
mabasi hayo.”
Baadhi
ya madereva wa Uda wamedaiwa kukatiza ‘ruti’ kwa lengo la kukusanyia fedha
nyingi.
“Abiria
wanapata usumbufu ruti zinapokatizwa kwa kuwa hawafahamu mwanzo na mwisho wa
maeneo ya safari zao,” alisema.
Ofisa
wa Uda, Henry Bantu alipoulizwa kuhusu kupokea amri hiyo, hakuwa tayari
kuelezea kwa kirefu akidai kwamba yeye siyo msemaji wa shirika.
“Mimi
siyo msemaji, lakini nachoweza kukueleza ni kwamba tuko kwenye mchakato wa
kuboresha huduma zetu,” alisema Bantu.
Tofauti
na mabasi mengine yanayotoa huduma za usafiri Dar es Salaam kupangiwa rangi
maalumu pamoja na kuandikwa maeneo ya safari zao mbele na mlangoni kuandikwa
kiwango cha nauli, mabasi ya Uda hayana utaratibu huo.
Wakati
huohuo, Ngowi amesema wamezifungia daladala 13 kutokana na kuwa kwenye hali ya
uchakavu kiasi cha kutishia usalama wa abiria.
Alisema
kiutaratibu, mabasi yanayotoa huduma lazima yawe kwenye hali nzuri ya usalama
ili kuepusha usumbufu kwa abiria na hata kusababisha ajali.
“Hatutakubali
kuona mabasi ya daladala yasiyokidhi sheria na taratibu za kubeba abiria
yakiendelea kutoa huduma jijini Dar es Salaam,” alisema Ngowi.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “UDA ZINAZOKATIZA SAFARI DAWA IMEIVA”
Post a Comment