Thursday, December 18, 2014
TATIZO LA WAMACHINGA NA OMBA OMBA MAENEO YASIYORUHUSIWA DAR KUTAFUTIWA DAWA .
Do you like this story?
Aron Msigwa –MAELEZO.
Jiji la Dar es salaam linaangalia upya utaratibu wa kuwaondoa ombaomba na
wafanyabiashara ndogondogo(wamachinga) katika maeneo yasiyoruhusiwa
katika jiji la Dar es salaam kufuatia sheria na hatua zinazochukuliwa ikiwemo
kuwarudisha ombaomba hao katika mikoa wanayotoka kutokuzaa matunda na kuwa
endelevu kufuatia wengi wao kurudi katika maeneo ya awali kila wanapoondolewa.
Hayo yamebainishwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Said Mecki Sadiki
wakati akifungua kikao cha wajumbe wa Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Dar es
salaam (RCC) kilichofanyika leo jijini Dar es salaam kujadili masuala
mbalimbali ya mendeleo katika jiji la Dar es salaam.
Amesema kuwa kuendelea kuwepo kwa wafanyabiashara hao katika maeneo
yasiyo rasmi ni moja ya changamoto inayolikabili jiji la Dar es salaam kutokana
na biashara wanazozifanya kuchangia kuzuia maeneo ya barabara ya waenda kwa
miguu, kusababisha uchafuzi wa mazingira,kusabisha msongamano wa magari kwa
baadhi yao kuweka bidhaa barabarani.
Amesema kutokana na hali hiyo baadhi ya wafanyabiashara walio na biashara
rasmi ambao hulipa kodi za Serikali wamekuwa wakilamikia hali ya
ukwepaji wa kodi inayofanywa na wafanyabiashara hao.
Bw. Sadiki amesema mpango wa mkoa wa sasa ni kuendelea kuwatumia
wafanyabiashara hao kama fursa ya mtaji wa rasilimali watu ambayo
itatumika kama chanzo cha mapato katika kuleta maendeleo ya mkoa.
Amesema watendaji na viongozi wa halmashauri za mkoa wa Dar es salaam
wanalojukumu la kuweka mazingira mazuri ya kufanya shughuli zao na kuwatumia
katika shughuli za uzalishaji kwa utaratibu mzuri utakaowekwa ili waendelee
kunufaika na shughuli wanazofanya.
Akizungumzia kuhusu uboreshaji wa huduma za jamii zikiwemo za Maji, Elimu
na Afya katika jiji la Dar es salaam amesema kuwa Serikali inaendelea
kuzijengea uwezo shule kwa kuongeza majengo ya madarasa, maabara na kuhakikisha
kuwa wanafunzi wote wanaofaulu elimu ya msingi wanapata fursa ya kuendelea na
masomo ya Sekondari.
Kuhusu huduma za afya amesema kuwa mkoa unaendelea na maandalizi ya
ujenzi wa jengo la ghorofa nane, eneo la Magomeni katika manispaa ya Ilala
litakalotumika kutolea huduma ya Afya ya Mama na Mtoto na kuwa na uwezo wa
kulaza wagonjwa 500.
“ Sasa tuko kwenye maandalizi ya ujenzi wa jengo maalum la kutolea
huduma ya Afya ya Mama na Mtoto katika jiji la Dar es salaam litakalogharimu
zaidi ya shilingi bilioni ishirini na moja, tayari benki ya Tanzania Investment
Bank imeshakubali kutoa mkopo kwa ajili ya jengo hilo” Amesisitiza.
Aidha, katika hatua nyingine Mkuu wa mkoa wa Dar es salaam ametoa
ufafanuzi kuhusu uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliofanyika nchi nzima
Desemba 14 mwaka huu na kueleza kuwa baadhi ya maeneo ya jiji la Dar es salaam
ambayo uchaguzi huo uliahirishwa kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo vurugu,
uchaguzi huo utarudiwa ndani ya siku saba.
Ameeleza kuwa katika mkoa wa Dar es salaam uchaguzi huo ulitarajiwa
kufanyika kwenye mitaa 561 lakini kutokana na changamoto mbalimbali ulifanyika
kwenye mitaa 491 na kuahirishwa kwenye kata 70.
Amelitaka jeshi la Polisi kuhakikisha kuwa linaimarisha ulinzi na usalama
wakati wa marudio ya uchaguzi huo unaotarajiwa kufanyika ndani ya siku 7 katika
mitaa yote ambayo uchaguzi uliahirishwa .
Subscribe to:
Post Comments (Atom)


.gif)


0 Responses to “ TATIZO LA WAMACHINGA NA OMBA OMBA MAENEO YASIYORUHUSIWA DAR KUTAFUTIWA DAWA .”
Post a Comment