Thursday, February 12, 2015
DAFTARI LA KUDUMU LA WAPIGA KURA SASA KUANZA KUBORESHWA KUANZIA JUMATATU FEBRUARI 16
Do you like this story?
SASA ni rasmi kwamba kazi ya
kuliboresha Daftari la Kudumu la Wapigakura nchini kote, itaanza Jumatatu ijayo
Februari 16 na kumalizika Aprili 29 mwaka huu.
Uandikishaji huo utaanzia katika mikoa
ya Lindi, Ruvuma, Mtwara na Njombe na baadaye utahamia katika mikoa mingine.
Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imesema
ratiba ya upigaji wa kura ya maoni ambayo ni Aprili 30 iko pale pale, kama
ilivyotangazwa na Rais Jakaya Kikwete. Wakati uandikishaji huo ukianzia katika
mikoa minne, utafungwa kwa kumalizia Dar es Salaam na Zanzibar.
Akizungumza jana ofisini kwake, Mkuu wa
Idara ya Elimu ya Mpiga Kura na Habari wa NEC, Ruth Masham aliwataka wananchi
kujitokeza kwa wingi katika uboreshaji wa daftari la wapigakura baada ya utoaji
wa elimu kwa waratibu kukamilika.
Alisema tume hiyo imetoa elimu kwa
waratibu wa waandikishaji kwa kila mkoa na katika kila mkoa wametoa mafunzo
hayo kwa mratibu mmoja.
Pia, elimu imetolewa kwa maofisa
waandikishaji wa Halmashauri, na wasaidizi wao na hao ndio watakaotumika kutoa
elimu kwa waandikishaji wadogo katika ngazi za tarafa na kata.
Masham alisema ni haki ya kila
Mtanzania kujiandikisha. Alisema wananchi wana haki ya kutumia fursa hiyo ya
kujiandikisha ili ifikapo Oktoba mwaka huu waweze kutumia haki hiyo ya kikatiba
kuchagua viongozi wanaowataka.
“Kila Mtanzania atapata fursa ya
kujiandikisha na kupata kitambulisho chake ambacho atakitumia wakati wa kupiga
kura. Hivyo tunawaasa watanzania wote wanaposikia uboreshaji umefika katika eneo
lake ajitokeze kujiandikisha,” alisema.
Katika kikao cha Bunge kilichomalizika
wiki iliyopita, Waziri Mkuu Mizengo Pinda aliwahakikishia Watanzania kuwa
uandikishwaji wa wapiga kura ambao utatumia Mfumo wa Kielektroniki (BVR),
utafanyika kwa ufanisi na kwa wakati uliopangwa.
Akijibu swali la Kiongozi wa Kambi
Rasmi ya upinzani Bungeni, Freeman Mbowe kuhusu uhakika wa uandikishaji huo,
Pinda alisema tume ya uchaguzi inaamini kuwa vifaa vitakavyotumika, vina ubora
mara mbili ya vilivyoletwa kwa ajili ya uandikishaji wa majaribio.
Licha ya kukiri kuwa awali serikali
ilikuwa na tatizo la kifedha, Pinda alisema tume imewahakikishia kuwa shughuli
zote za upigaji kura kwa ajili ya Katiba Inayopendekezwa na uchaguzi mkuu,
zitafanyika.
Pinda alimtoa wasiwasi Mbowe kuhusu
ufanisi wa vifaa hivyo vya BVR, kwa kusema endapo tume itaona kuwa uandikishaji
huo hauwezekani kwa sababu yoyote ile, itatoa taarifa bungeni na serikali iko
tayari kubadili maamuzi.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “DAFTARI LA KUDUMU LA WAPIGA KURA SASA KUANZA KUBORESHWA KUANZIA JUMATATU FEBRUARI 16 ”
Post a Comment