Wednesday, February 25, 2015

PATO LA MWANANCHI MBEYA LAVUKA LENGO LA KITAIFA





WAZIRI
MKUU Mizengo Pinda ameupongeza uongozi wa mkoa wa Mbeya kwa kuvuka lengo la wastani
wa pato la mwananchi kitaifa na kuwataka waendeleze kasi ya kupambana na
umaskini kwa wakazi wa mkoa huo.


Ametoa
pongezi hizo jana wakati akizungumza na
viongozi wa mkoa huo na wilaya zote wakiwemo wadau mbalimbali na viongozi wa
dini mara baada ya kupokea taarifa ya Mkoa wa Mbeya.


Alisema
katika mipango yake, Serikali ililenga kwamba pato la mtu kwa mwaka liwe sh.
1,186, 200, lakini kwa sababu ya jitihada mbalimbali mkoa huo umelivuka. “Katika
taarifa aliyonisomea, Kaimu Mkuu wa Mkoa amesema wastani wa pato la mwananchi umeongezeka
kutoka sh. 711,201/- mwaka 2008 hadi kufikia sh 1,420,427/- mwaka 2013 na
kwamba mkoa unachangia asilimia 7.43 ya Pato la Taifa,” alisema.


Alisema
kipato cha mtu mmoja kwa siku ni sh. 3,891/- ambazo ni zaidi ya Dola mbili za
Marekani (sh. 3,400/-). “Wakubwa hawa wanatupima kwa kuangalia kipato cha mtu
kwa siku. Wanasema nchi ni maskini iwapo watu wake wanaishi chini ya dola moja
kwa siku (sawa na sh. 1,700/-).

“Mbeya
imeendelea kushika nafasi ya tatu kwa kuchangia vizuri Pato la Taifa ikiwa
imetanguliwa na Dar es Salaam na Iringa. Ninawapongeza kwa sababu mmevuka
malengo ya Taifa katika eneo la pato la mtu mmoja mmoja,” alisema Waziri Mkuu.

Mapema, Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Bw.
Deodatus Kinawilo ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Chunya, alisema pato la mkoa limeongezeka
kutoka sh. trilioni 1.779 mwaka 2008 na kufikia sh. trilioni 3.951 mwaka
2013. 

“Uchumi
wa mkoa huu unategemea kilimo, ufugaji, uchimbaji madini, uvunaji mazao ya
maliasili, biashara, uzalishaji viwandani na ajira katika taasisi za serikali
na sekta binafsi,” alisema.


Wakati huohuo, uongozi wa mkoa wa Mbeya umetakiwa kuongeza
bidii ili uweze kuinua kiwango cha ufaulu wa elimu ya kwa sababu umekuwa
ukiendelea kushuka na kuwa chini ya kiwango cha asilimia 60 kilichowekwa na Serikali
Wazir
Mkuu aliutaka uongozi huo ubuni mbinu za kisomi zitakazowawezesha wanafunzi wa
shule za msingi kuelewa wanachofundishwa, hivyo, kufaulu mitihani yao vizuri. ”Ufaulu
wenu kwa shule za msingi ni asilimia 46.6, uko chini ya kiwango cha kitaifa cha
ufaulu kwa asilimia 13.4. Ni matokeo yasiyoridhisha, fanyeni utaratibu maalum ili
yapande,” alisema.

0 Responses to “PATO LA MWANANCHI MBEYA LAVUKA LENGO LA KITAIFA ”

Post a Comment

More to Read