Saturday, February 20, 2016
CHATU AZUA KIZAAZAA SONGEA
Do you like this story?
SONGEA: WAKAZI wa Mtaa wa Matuli Kata ya
Majengo na Mfaranyaki-Makaburini, Manispaa ya Songea, mkoani Ruvuma, wameingiwa
na hofu ya usalama wa maisha yao baada ya kuonekana kwa chatu anayezunguka
katika pori la mto unaotenganisha maeneo hayo.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na waandishi
wa habari mjini hapa, wananchi hao walisema kuwa chatu huyo ameonekana zaidi ya
mara tatu kwa nyakati tofauti tangu wapate taarifa ya uwepo wa chatu huyo
katika maeneo hayo hali inayosababisha shughuli za kilimo katika bonde la Mto
Ruvuma kusimama.
Kama hiyo haitoshi, chatu huyo amesababisha
baadhi ya wanafunzi kushindwa kuhudhuria masomo kutokana na kuhofia usalama
wao.
Fatuma Omary na Zainabu Msangu, wakazi wa
Majengo, Mtaa wa Matuli walisema kuwa mwenyekiti wa serikali ya Mtaa wa
Mfaranyaki aliwatahadharisha wananchi kuwa ofisi yake imepokea taarifa ya
kuwepo kwa chatu mkubwa katika bonde la Majengo na kuwataka wawe makini
wanapotembea na kufanya shughuli za kilimo.
Aidha, Afisa Mifugo, Aletas Kapinga anayeishi
katika bonde hilo, aliwaomba maafisa wanyamapori kutumia ujuzi walionao
kumtafuta nyoka huyo anayetishia maisha ya wananchi na mifugo yao kwani
shughuli za kilimo na bustani zimesimama.
Kufuatia tukio hilo inadaiwa kuwa mbwa watatu
pamoja na kuku wawili wamekamatwa na kumezwa na chatu huyo jambo
linalosababisha watoto kukatazwa kwenda kuchota maji kwenye bonde hilo na
wengine kushindwa kwenda kumwagilia bustani zao.
Kwa upande wake, Afisa Wanyamapori wa Wilaya
ya Songea, Oscar Bakumbezi amethibitisha kuwa ofisi yake imepokea taarifa toka
kwa wananchi wa maeneo hayo kuhusu uwepo wa chatu huyo na kwamba amekwisha
kamata mbwa watatu na kuku wawili na tayari hatua mbalimbali zimechukuliwa
ikiwa ni pamoja na kufanya doria ya kumsaka nyoka huyo na amewataka wananchi
kufanya usafi wa mazingira kwa kufyeka nyasi kwenye maeneo yote yanayozunguka
nyumba zao.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “ CHATU AZUA KIZAAZAA SONGEA”
Post a Comment