Tuesday, March 18, 2014
HOTUBA YA JAJI JOSEPH WARIOBA ALIYOSOMA KWENYE BUNGE MAALUM LA KATIBA LEO.
Do you like this story?
HOTUBA YA
MWENYEKITI WA TUME YA MABADILIKO YA KATIBA, MHE. JAJI
JOSEPH SINDE WARIOBA, AKIWASILISHA RASIMU YA KATIBA YA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KATIKA BUNGE MAALUM LA KATIBA, MACHI
2014 ________________ UTANGULIZI
Mheshimiwa
Mwenyekiti.
Waheshimiwa
Wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba,
Kwa mujibu wa kifungu 20 (3) cha
Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, Sura ya 83 na Tangazo la Serikali Na. 30 la
tarehe 14 Februari, 2014, naomba kuwasilisha Rasimu ya Katiba kwenye Bunge
Maalum la Katiba. Rasimu ya Katiba ninayoiwasilisha imeandaliwa na Tume ya
Mabadiliko ya Katiba baada ya kukamilisha kazi ya kuratibu, kukusanya,
kuchambua na kutathmini maoni ya wananchi kuhusu Katiba Mpya. 2.
Mwanzo kabisa, nieleze kwamba,
Maelezo haya ninayoyatoa, ni sehemu ya Randama (Memorandum) iliyoandaliwa na
Tume kwa lengo la kufafanua kwa kina, maudhui
ya kila Ibara iliyomo katika Rasimu ya Katiba na sababu za mapendekezo ya
Ibara hizo. Hivyo, naomba maelezo yote yaliyomo katika Randama yawe sehemu ya
maelezo yangu na yaingizwe katika kumbukumbu za Bunge hili. 3.
Rasimu ya Katiba ni miongoni mwa
Nyaraka zilizoambatanishwa katika Ripoti ya Tume kuhusu Mchakato wa Mabadiliko
ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tuliyowakabidhi Waheshimiwa Marais
tarehe 30 Desemba, 2013. Nyaraka nyingine ni:
Taarifa ya Maoni ya Wananchi kuhusu Mabadiliko
ya Katiba. Taarifa hii ina maoni ya Wananchi kuhusu maeneo mbalimbali ya
kikatiba ambayo ndio msingi wa uandishi wa Rasimu ya Katiba; (b)
Taarifa ya Mabaraza ya Katiba ambayo
inaainisha maoni ya Wananchi kuhusu Ibara zilizokuwemo katika Toleo la Kwanza
la Rasimu ya Katiba na jinsi zilivyofanyiwa kazi; (c)
Taarifa ya maoni ya Wananchi kuhusu Sera,
Sheria na Utekelezaji. Taarifa hii ina maoni ya wananchi kuhusu mambo ambayo
yanahitaji kufanyiwa uamuzi wa kisera, kutunga au kurekebisha sheria zilizopo
au utekelezaji wa kiutendaji; (d)
Taarifa ya Utafiti Kuhusu Masuala
Mbalimbali ya Kikatiba, ambayo ina taarifa nne ambazo ni: (i)
Utafiti Kuhusu Madaraka ya Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; (ii)
Utafiti Kuhusu Maadili ya Viongozi
na Uwajibikaji; (iii)
Utafiti Kuhusu
Masuala Yanayohusu Muungano wa Tanganyika na Zanzibar;
na (iv)
Ushauri Elekezi Kuhusu Mifumo ya
Uchaguzi na Tume ya Uchaguzi, Tanzania (Final Report on the Review of Various
Aspects of Electoral Systems and the Electoral Commission in Tanzania).
(e)
Taarifa ya Takwimu za Ukusanyaji wa
maoni ya Wananchi ambayo inaainisha maeneo makuu yaliyotolewa maoni, jinsi,
elimu na kazi za watoaji maoni; na (f)
Viambatisho vya Ripoti ambavyo
vinaainisha hatua mbalimbali za mchakato, uamuzi, hotuba za viongozi na
miongozo mbalimbali iliyotolewa na Tume. 4.
Ripoti ya Tume na baadhi ya Taarifa
zimegawiwa kwa kila Mjumbe na Taarifa nyingine zimewekwa katika Maktaba ya
Bunge ili kuwawezesha Wajumbe kufanya marejeo. Tume inaamini kwamba Ripoti na
Taarifa zinazowasilishwa pamoja na maelezo haya zitawasaidia Wajumbe wa Bunge
Maalum la Katiba kujadili na kufanya uamuzi sahihi kwa kila Ibara
iliyopendekezwa kwa kuzingatia maslahi ya wananchi na Taifa kwa jumla
Rais, atabaki
na madaraka ya kuwateua viongozi wa kitaifa, kama vile Mawaziri, Majaji, Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama, Makatibu
Wakuu wa Wizara na Wenyeviti na Wajumbe wa Tume za kitaifa. Pamoja na kubaki na
madaraka hayo, Rais amewekewa utaratibu wa uteuzi. Baadhi ya viongozi
watateuliwa moja kwa moja na Rais na baadaye watathibitishwa na Bunge, kwa
mfano, Mawaziri. Wengine watapendekezwa na Kamati ya Uteuzi na baada ya
kuteuliwa, watathibitishwa na Bunge, kwa mfano, Mwenyekiti na Wajumbe wa Tume
Huru ya Uchaguzi. Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama watateuliwa na Rais kwa
kushauriana na Baraza la Ulinzi na Usalama la Taifa. Wengine watateuliwa kutokana
na ushauri wa Tume za Utumishi, kama vile Majaji na Makatibu Wakuu.
Bunge
Mheshimiwa
Mwenyekiti;
Kwa Bunge la Muungano, madaraka yake
na mamlaka yatabaki kusimamia mambo ya Muungano. Kinachobadilika sasa ni Bunge
kutokuwa na mamlaka juu ya mambo yasiyo ya
Muungano ya Tanganyika kama ambavyo imekuwa kwa upande wa Zanzibar. Hata
hivyo, Bunge la Muungano litapata taarifa ya uratibu na utekelezaji wa mambo
yasiyo ya Muungano ya Tanganyika na ya Zanzibar kupitia Tume ya Uhusiano na
Uratibu wa Serikali
Imependekezwa pia kwamba Spika na
Naibu Spika wasitokane na Mawaziri, Naibu Mawaziri au Wabunge. Lengo la
pendekezo hili ni kupata viongozi ambao wataonekana hawaegemei upande wowote.
Imependekezwa pia kwamba Wabunge wasiwe Mawaziri. Pendekezo hili limetokana na
maoni ya wananchi
kwamba wanahitaji Wabunge kuwa karibu
na wapiga kura wao. Wengine wanaamini kwamba wabunge ambao ni Mawaziri
wanapendelea majimbo yao ya uchaguzi badala ya kutumikia taifa kwa ujumla kwa
usawa.
Lakini lengo jingine la pendekezo
hili, ni kutenganisha madaraka ya mihimili. Kama Bunge likiwa na madaraka ya
kuthibitisha Mawaziri itakuwa vigumu kwa Wabunge kuwakataa Wabunge wenzao
watakaoteuliwa kuwa Mawaziri, kisha kuendelea kukaa pamoja kwa utulivu ndani ya
Bunge
Tume imependekeza ukomo wa ubunge
kuwa vipindi vitatu vya miaka mitano mitano.
Hata hivyo, wananchi wanaweza kumwondoa Mbunge wao kabla ya kumaliza muda
wa kipindi chake cha miaka mitano. Pendekezo hili linatokana na maoni ya
wananchi waliotaka kuwepo ukomo wa ubunge ili kuondoa dhana ya umiliki wa jimbo
la uchaguzi, kutoa fursa kwa wananchi wengine wenye uwezo kugombea nafasi ya
ubunge, kuongeza uwajibikaji wa wabunge katika majimbo ya uchaguzi na kuongeza
mamlaka ya wananchi kuwawajibisha viongozi wao.
Pia, ni maoni ya wananchi kuwa
kusiwepo uchaguzi mdogo ili kupunguza gharama. Endapo nafasi ya ubunge itaachwa
wazi kutokana na mbunge wa chama cha siasa kupoteza Ubunge, basi Tume Huru ya
Uchaguzi itajaza nafasi hiyo kutokana na orodha ya majina yaliyowasilishwa na
chama cha siasa husika na kwa kushirikiana na chama hicho. Uchaguzi mdogo
utafanyika tu pale ambapo nafasi ya ubunge iliyo wazi imetokana na mbunge huru.
Mahakama
Kuhusu
Mahakama, pendekezo kubwa ni kuundwa kwa Mahakama ya Juu na kwamba Mahakama hiyo na Mahakama ya Rufani ndizo ziwe
Mahakama za Muungano. Mahakama Kuu ziendelee kutokuwa za Muungano kama ilivyo
sasa. Hata hivyo, inapendekezwa kuwa Mahakama Kuu ya Tanganyika na Mahakama Kuu
ya Zanzibar ziwe na mamlaka sawa katika kusikiliza na kuamua mashauri yanayohusu
masuala ya Muungano na yasiyo ya Muungano (concurrent jurisdiction). Hivi
ndivyo ilivyo hivi sasa kwa upande mmoja, ambapo Mahakama Kuu ya Zanzibar,
japokuwa si sehemu ya Mahakama za Jamhuri ya Muungano, lakini imepewa mamlaka
na Katiba ya Jamhuri ya Muungano kusikiliza na kuamua kuhusu mashauri ya kesi
za madai na jinai yanayohusu sheria za muungano. Pendekezo jingine ni kuuweka
Mfuko wa Mahakama ndani ya Katiba.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “HOTUBA YA JAJI JOSEPH WARIOBA ALIYOSOMA KWENYE BUNGE MAALUM LA KATIBA LEO.”
Post a Comment