Thursday, March 20, 2014
MIRADI KUKABILI FOLENI YASUASUA.
Do you like this story?
Kasi ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya
kupunguza msongamano wa magari jijini Dar es Salaam inaonekana si ya kuridhisha
licha ya ukubwa wa tatizo lenyewe.
Miradi hiyo ilitangazwa bungeni na Waziri wa
Ujenzi, Dk. John Magufuli katika hotuba yake ya Bajeti ya Mwaka 2013/2014.
Baadhi ya miradi iliyotangazwa na waziri ni
pamoja na ujenzi wa barabara za juu kwenye makutano ya barabara
(flyover).
Mradi huu bado haujaanza kutekelezwa licha ya
Dk. Magufuli kulieleza Bunge kuwa wakati ule walikuwa katika mchakato wa
kumpata mkandarasi.
Mradi mwingine ni ujenzi wa kivuko au boti
kutoka Dar es Salaam mpaka Bagamoyo chenye uwezo wa kubeba watu 300.
Mradi huu pia ungesaidia kwa kiasi kikubwa
kupunguza msongamano kwani baadhi ya watu wangesafiri kwa kutumia kivuko au
boti maalumu mpaka Bagamoyo.
Dk. Magufuli alisema katika hotuba yake kuwa
mkandarasi wa mradi huo alikuwa amepatikana na usanifu wa maegesho matatu
ulikuwa unaendelea.
Mpaka sasa hamna shughuli zozote zinazohusu
mradi huo zinazoendelea, licha ya tamko hilo kutolewa na waziri mwenyewe.
Meneja wa Tanroads Mkoa wa Dar es Salaam,
Julius Ndyamkama alisema ujenzi wa kivuko unaendelea mjini Bangladesh, India na
mwezi wa tano kivuko hicho kitawasili nchini.
Ndyamkama alisema Tanroads wameanza
maandalizi ya ujenzi wa Flyover maeneo ya Tazara na mpaka sasa wameondoa
mabango ya matangazo, mabomba na nguzo za umeme eneo ambako litajengwa
daraja la juu.
“Kuhusu barabara alizozisema waziri, tayari
makandarasi wameshapatikana na mikataba yote tuliyoingia ipo kwa Mwanasheria
Mkuu. Utekelezaji utaanza baada ya Mwanasheria Mkuu kupitia mikataba hiyo,”
alisema Ndyamkama.
Tatizo la msongamano wa magari Dar es
Salaam limeongezeka zaidi kutokana na sababu mbalimbali zikiwamo
ujenzi wa mradi mwingine wa barabara za Mabasi Yaendayo Kasi (Dart).
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “MIRADI KUKABILI FOLENI YASUASUA.”
Post a Comment