Thursday, March 20, 2014
JAZIBA IEPUKWE KATIKA KUJADILI RASIMU YA KATIBA.
Do you like this story?
Hatimaye Rasimu ya Pili ya Katiba
iliwasilishwa bungeni jana baada ya kutokea sintofahamu juzi na
kusababisha kusitishwa kwa kikao cha Bunge Maalumu la Katiba pasipo
Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba kuiwasilisha
bungeni kama ilivyokuwa imepangwa. Mtafaruku huo ulitokea baada ya baadhi ya
wajumbe kupinga kuruhusiwa kwa Jaji Warioba kuwasilisha Rasimu hiyo kabla Rais
Jakaya Kikwete hajalihutubia Bunge kama Kanuni za Bunge zinavyoelekeza.
Kuwasilishwa kwa Rasimu hiyo jana kulitokana
na kupatikana kwa maridhiano juzi usiku kati ya uongozi wa Bunge na viongozi wa
Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), unaovishirikisha vyama vya upinzani na
wajumbe wanaotokana na makundi yaliyotajwa katika kifungu cha 22(1)(C) cha
Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, Sura ya 83. Umoja huo ulianzishwa kwa lengo la
kuhakikisha mchakato wa Katiba unaiwezesha nchi yetu kupata Katiba Mpya na
iliyo bora.
Ni vigumu kuelezea ukubwa wa vurugu zilizotokea
bungeni juzi kutokana na ufinyu wa nafasi katika safu hii. Hata hivyo, viongozi
wa Ukawa walitangaza mapema juzi kwamba wangepinga, pamoja na mambo mengine,
ukiukwaji wa Kanuni na wangezuia ratiba kuendelea hadi kwanza yasikilizwe
madai yao ya kumtaka Rais Kikwete afungue Bunge kabla ya kuwasilishwa kwa
Rasimu ya Katiba.Ndiyo maana Jaji Warioba aliposimama kwenye mimbari ya Bunge
tayari kuwasilisha Rasimu hiyo, baadhi ya wajumbe walipiga kelele na kugonga
meza, hivyo kumfanya ashindwe kufanya kazi hiyo. Kama tulivyodokeza hapo juu,
uwasilishaji huo ulifanyika jana baada ya maridhiano kupatikana.
Sisi hatuwezi kuunga mkono vurugu Bungeni
lakini tunadhani kwamba tukio hilo litakuwa limetoa fundisho kwa Mwenyekiti wa
Bunge kwamba kamwe hataweza kuongoza chombo hicho pasipo kufuata Kanuni
zilizotungwa kuendesha shughuli zake.
Mwenyekiti huyo anapaswa kujua kwamba
alivunja Kanuni ya 7(1)(g) na (h) ambazo zimeweka mpangilio wa shughuli zote za
Bunge la Katiba. Ratiba hiyo ilionyesha wazi kwamba hotuba ya ufunguzi ambayo
itatolewa na Rais, itatangulia na kufuatiwa na uwasilishaji wa Rasimu ya
Katiba.
Tunashawishika kusema ukiukwaji huo wa Kanuni
ulifanywa kwa makusudi, hasa tukizingatia uzoefu alioupata akiwa Spika wa
Bunge la Tisa la Jamhuri ya Muungano. Yatakuwa makosa makubwa iwapo atadhani
kwamba makundi yenye wajumbe wachache yatakubali kuburuzwa, kwani Bunge la
Katiba ni tofauti na Bunge la kawaida ambalo limekuwa na dhana potofu kwamba
kundi lenye wabunge wengi ndilo lina haki ya kusikilizwa.
Tunakubaliana na
viongozi wa Ukawa wanapohadharisha kwamba Katiba hii itatumiwa na vizazi na
vizazi, hivyo ni lazima itengenezwe kwa misingi ya kujali utu wa kila mtu,
kuheshimiana na kukubaliana.
Ubabe na kukiuka Kanuni kwa kisingizio cha
‘busara za Mwenyekiti’ havikubaliki, isipokuwa tu pale Kanuni zinapokuwa
hazielekezi chochote.
Tukio kubwa lililokuwa likisubiriwa ni
uwasilishwaji wa Rasimu ya Katiba ambao ulifanywa jana na Jaji Warioba kwa
utulivu, umakini, busara na ustadi mkubwa.
Alipewa muda wa kutosha kutoa ufafanuzi wa
masuala mazito na alifanya hivyo bila ya kuwaburuza. Wajumbe sasa wanayo Rasimu
mbele yao ambayo watapaswa kuijadili bila ya jazba, bali kwa kuzingatia hoja
badala ya kuangalia nani anatoa hoja.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “JAZIBA IEPUKWE KATIKA KUJADILI RASIMU YA KATIBA.”
Post a Comment