Thursday, May 15, 2014

JUKUMU LA UOKOAJI KUKABIDHIWA JWTZ.




Serikali imeliambia Bunge kuwa, iko katika mchakato wa kuifanyia marekebisho Sheria ya Maafa ili kuliondoa suala la uokoaji kutoka Jeshi la Zimamoto kwenda Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi alisema juzi kuwa katika mabadiliko hayo ya sheria, JWTZ litakabidhiwa dhamana pia ya kufanya uokoaji majini na nchi kavu. Lukuvi alitoa kauli hiyo wakati akifafanua swali la Mbunge wa Kuteuliwa, James Mbatia aliyetaka kufahamu Serikali ina mpango gani wa kuipatia JWTZ, vifaa na teknolojia ya kisasa ya uokoaji.

Mbunge huyo aliomba ufafanuzi huo wakati Bunge lilipoketi kama kamati, kupitia Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na JKT kwa mwaka wa fedha wa 2014/15.

Mbatia alirejea matukio mbalimbali ya maafa, yakiwamo mafuriko na kuanguka kwa jengo la ghorofa Dar es Salaam ambako JWTZ lilishiriki katika uokoaji kwa kutumia vifaa duni.

“Jeshi letu kwa hali tuliyonayo sasa, waziri anasemaje kuwa na vifaa na teknolojia ya kisasa ili maafa yanapotokea wasitumie mtulinga,” alihoji.
Swali hilo lilijibiwa na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk Hussein Mwinyi aliyesema tayari wana mpango wa kukiimarisha Kitengo cha Uhandisi cha Jeshi ili kiwe na vifaa vya kisasa vya uokoaji.

Katika nyongeza ya majibu ya swali hilo, ndipo Lukuvi aliposimama na kusema ingawa ipo Sheria ya Maafa, imekuwa haisaidii, hivyo Serikali inaifanyia marekebisho ili JWTZ ikabidhiwe dhamana ya uokoaji.

“Kwa sasa unaweza kuona suala hili la uokoaji linafanywa na Zimamoto ambao kisheria ndiyo wanaosimamia zimamoto na uokoaji, lakini mara nyingi tumekuwa tukitumia Jeshi... “Kwa hiyo tunataka tuwape uwezo wa kisheria wa kushughulikia mambo kama hayo baharini na uokoaji kama huu ambao utawezesha jeshi lenyewe kuwa na bajeti ya kufanya mambo hayo kuliko ilivyo sasa wanajiminya kwenye bajeti zao kwa mambo ambayo kwa kweli hayako ndani ya sheria.

Kauli hiyo ya Serikali kukabidhi shughuli za uokoaji kwa JWTZ, imekuja wakati kukiwa na mapendekezo ya wadau mbalimbali kutaka Jeshi la Zimamoto na Uokoaji liwe sehemu ya Jeshi la Polisi.
Hoja hiyo inatokana na ukweli kwamba, mara zote kwenye matukio ya moto, polisi ndiyo wanakuwa wa kwanza kufika, hivyo Zimamoto ikiingizwa huko, uokoaji utafanyika sambamba na kazi za ulinzi.

0 Responses to “JUKUMU LA UOKOAJI KUKABIDHIWA JWTZ.”

Post a Comment

More to Read