Thursday, May 15, 2014
JUKUMU LA UOKOAJI KUKABIDHIWA JWTZ.
Do you like this story?
Serikali
imeliambia Bunge kuwa, iko katika mchakato wa kuifanyia marekebisho Sheria ya
Maafa ili kuliondoa suala la uokoaji kutoka Jeshi la Zimamoto kwenda Jeshi la
Wananchi wa Tanzania (JWTZ).
Waziri
wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi alisema
juzi kuwa katika mabadiliko hayo ya sheria, JWTZ litakabidhiwa dhamana pia ya
kufanya uokoaji majini na nchi kavu. Lukuvi alitoa kauli hiyo wakati akifafanua
swali la Mbunge wa Kuteuliwa, James Mbatia aliyetaka kufahamu Serikali ina
mpango gani wa kuipatia JWTZ, vifaa na teknolojia ya kisasa ya uokoaji.
Mbunge
huyo aliomba ufafanuzi huo wakati Bunge lilipoketi kama kamati, kupitia
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na JKT kwa mwaka wa fedha
wa 2014/15.
Mbatia
alirejea matukio mbalimbali ya maafa, yakiwamo mafuriko na kuanguka kwa jengo
la ghorofa Dar es Salaam ambako JWTZ lilishiriki katika uokoaji kwa kutumia
vifaa duni.
“Jeshi
letu kwa hali tuliyonayo sasa, waziri anasemaje kuwa na vifaa na teknolojia ya
kisasa ili maafa yanapotokea wasitumie mtulinga,” alihoji.
Swali
hilo lilijibiwa na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk Hussein
Mwinyi aliyesema tayari wana mpango wa kukiimarisha Kitengo cha Uhandisi cha
Jeshi ili kiwe na vifaa vya kisasa vya uokoaji.
Katika
nyongeza ya majibu ya swali hilo, ndipo Lukuvi aliposimama na kusema ingawa ipo
Sheria ya Maafa, imekuwa haisaidii, hivyo Serikali inaifanyia marekebisho ili
JWTZ ikabidhiwe dhamana ya uokoaji.
“Kwa
sasa unaweza kuona suala hili la uokoaji linafanywa na Zimamoto ambao kisheria
ndiyo wanaosimamia zimamoto na uokoaji, lakini mara nyingi tumekuwa tukitumia
Jeshi... “Kwa hiyo tunataka tuwape uwezo wa kisheria wa kushughulikia mambo
kama hayo baharini na uokoaji kama huu ambao utawezesha jeshi lenyewe kuwa na
bajeti ya kufanya mambo hayo kuliko ilivyo sasa wanajiminya kwenye bajeti zao
kwa mambo ambayo kwa kweli hayako ndani ya sheria.
Kauli
hiyo ya Serikali kukabidhi shughuli za uokoaji kwa JWTZ, imekuja wakati kukiwa
na mapendekezo ya wadau mbalimbali kutaka Jeshi la Zimamoto na Uokoaji liwe
sehemu ya Jeshi la Polisi.
Hoja
hiyo inatokana na ukweli kwamba, mara zote kwenye matukio ya moto, polisi ndiyo
wanakuwa wa kwanza kufika, hivyo Zimamoto ikiingizwa huko, uokoaji utafanyika
sambamba na kazi za ulinzi.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “JUKUMU LA UOKOAJI KUKABIDHIWA JWTZ.”
Post a Comment