Saturday, October 11, 2014
WATAKAOFAULU KIDATO CHA KWANZA 2015 MKOANI NJOMBE WAKIWA HAWAJUI KUSOMA NA KUANDIKA KURUDISHWA NYUMBANI
Do you like this story?
CHANGAMOTO kubwa
inayoikabili sekta ya elimu nchini ya ukosefu wa ubora wa elimu, imelifanya
Baraza la Madiwani katika Halmashauri ya Wilaya ya Njombe kuingia kwenye orodha
ya Wilaya zinazotarajiwa kuleta mabadiliko katika sekta ya elimu nchini, baada
ya kupitisha azimio la kutaka maafisa elimu msingi na sekondari wilayani humo
kufanya usaili wa wanafunzi watakaofaulu kujiunga na elimu ya kidato cha kwanza
2015 unafanyika ili kubaini kama wanajua kusoma na kuandika au la.
Miongoni mwa maazimio
yaliyoafikiwa na madiwani hao ni pamoja na madiwani kuamua kuwabana
wazazi ambao watashindwa kupeleka watoto wao shule na kujua idadi ya wanafunzi
watakaofaulu mtihani wa taifa wa darasa la saba mwaka huu ili waweze kuhoji ufaulu
wao ulitokana na nini kama hawajui kusoma na kuandika.
Imeelezwa kuwa,
wakati wa maafikiano hayo baadhi ya madiwani walikataa kuafiki mkakati huo kwa
lengo la kuwalinda wakuu wa shule za msingi walioruhusu watoto kufanya mtihani
na endapo watafaulu wakati wakijua hawajui kusoma wala kuandika.
Wakizungumza kwa
masharti ya kutotajwa majina yao wajumbe wa Baraza la Madiwani wa Halmashauri
hiyo, wameeleza kuwa ni lazima maafisa elimu wote sekondari wahakikishe
wanapata miongozo kutoka Wizara ya Elimu na Mfunzo ya Ufundi ya jinsi ya
kusimamia zoezi hilo kwasababu ndiyo kazi yao.
Akizungumza mbele ya
Mkuu wa Wilaya hiyo, Sarah Dumba, diwani wa kata ya Ludewa, Monica Mchilo,
ameeleza kuwa siku maadhimio hayo yalipoafikiwa haitasahaulika mashani mwake
kwa yaliyotokea kutokana na baadhi ya wajumbe wa Baraza hilo kutaka
kuwakumbatia wakuu wa shule za msingi watakaobainika kuwa walifanya udanganyifu
wa namna ya kuwafaulisha wanafunzi huku wakijua kuwa hawana sifa stahiki.
Alisema chanzo cha
maamuzi hayo ni baada ya kutathimini hali ya taaluma katika Wilaya hiyo kuwa
hairidhishi, na baada ya kukatazwa kuwa wasizungumzie suala hilo baadhi ya
wajumbe wa baraza walijitenga.
Hata hivyo baada ya
kufikishwa taarifa hiyo kwa bodi ya wazazi, baadhi yao walipokea kwa furaha
suala hilo, huku wengi wao wakitaka umri wa wanafunzi kuanza shule uzingatiwe
kwani wengi wa wanafunzi wanaoanza shule za msingi wilayani humo wanachelewa
kuanza shule na kuwafanya kuwa na uelewa mdogo darasani na kushindwa kusoma
kabisa.
Baadhi ya wajumbe wa
bodi ya wazazi wameeleza kuwa mkakati wa madiwani hao hauna tatizo na kwamba
tatizo la wanafunzi kushindwa kusoma na kuandika linatokana na uongozi dhaifu
kuanzia ngazi ya familia hadi Wilaya ambapo walidai kuwa ukabila umeshamiri kwa
walimu kujiona kuwa kabila ama ukoo fulani haustahili kupata elimu iliyo bora.
Kwa upande wa Ofisi
ya Elimu Msingi wilayani humo, imesema kutokana na dhamira ya Baraza la
Madiwani hao ni lazima kila mwanafunzi atakayefaulu kujiunga na elimu ya kidato
cha kwanza atafanyiwa usaili huo. Pamoja na mambo mengine, imeelezwa kwamba
usaili huo utasimamiwa na walimu wakuu wa shule husika na kwamba mwanafunzi
atakayebainika kutojua kusoma au kuandika, atarejeshwa nyumbani.
via fikrapevu
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “WATAKAOFAULU KIDATO CHA KWANZA 2015 MKOANI NJOMBE WAKIWA HAWAJUI KUSOMA NA KUANDIKA KURUDISHWA NYUMBANI ”
Post a Comment