Monday, June 16, 2014

KITOKOLOLO RAPA WA FM ACADEMIA AHAMIA BENDI YA MASHUJAA.




BENDI ya Mashujaa imemchukua rapa, Kalidjo Kitokololo ‘Kuku’ kutoka bendi ya  FM Academia na kusaini naye  Mkataba wa miaka miwili.

Akizungumza kwenye ukumbi wa Milenium Business  Park leo , Kijitonyama, Dar es Salaam Mkurugenzi wa Mawasiliano wa bendi hiyo, Maximillian Luhanga amesema  kupatikana kwa  Chitokololo ni furaha kubwa kwao.

“Kalidjo anakuwa rapa wa tatu katika bendi ya Mashujaa , baada ya Saulo John maaurufu  Ferguson na Sauti ya Radi, ambao wote ni wakali, kwa marapa hao wote tunaamini bendi yetu itakuwa inatisha sana,”amesema Luhanga.
  
Maxmilian Luhanga  amesema Kitokololo anaanza kazi mara moja baada ya kusaini mkataba mpya.
Kwa upande wake, Kitokololo mwanamuziki kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) amesema  amekuja Tanzania kutafuta maisha na Mashujaa imempa ofa nzuri ndiyo maana amejiunga na bendi hiyo.

Amesema ameondoka vizuri FM Academia akiwa amewaaga vizuri wenzake ambao wameridhia kuondoka kwake.
  Kitokololo amesema kwamba amejiunga na Mashujaa akimfuata  King Dodo  ambaye kimuziki ni baba yake , King Dodoo  ndiye aliyemleta nchini kwa mara ya kwanza mwaka 2004.

Mashujaa itamtambulisha rasmi mwanamuziki huyo katika onyesho maalum litakalofanyika ukumbi wa Letasi Lounge Ijumaa wiki hii.
Mashujaa pia wanatarajiwa kuwa na ratiba ndefu mara baada ya mfungo mtukufu wa ramadhani ambapo Maximillian Luhanga amewaambia mashabiki wa bendi hiyo nchini kote kukaa mkao wa kula, Kwakuwa bendi hiyo itakuwa na ziara karibu mikoa yote ya Tanzania ili kutoa burudani kwa mashabiki wao.

0 Responses to “KITOKOLOLO RAPA WA FM ACADEMIA AHAMIA BENDI YA MASHUJAA.”

Post a Comment

More to Read