Tuesday, June 10, 2014

SERIKALI YATANGAZA KUKOMAA NA WANAOPIGA PICHA CHAFU NA KUZIWEKA KWENYE MITANDAO




SERIKALI imekemea tabia ya baadhi ya watu, wakiwemo wasanii kuweka kwenye mitandao picha chafu zinazokiuka maadili ya kitanzania na kusababisha mmomonyoko wa maadili. 


Naibu Waziri wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Juma Nkamia, ametoa kauli hiyo jana Juni 9, 2014 mjini Dododa na kusema kuwa serikali haifurahishwi na picha hizo, ambazo husambazwa kwenye mitandao na kuwataka Watanzania kujiepusha na tabia hiyo. 


Aidha, amekemea tabia ya baadhi ya wasanii wa filamu wanaotengeneza filamu zinazokuika maadili zikiwemo zinazowaonyesha wakiwa wamevaa mavazi yasiyo na staha. 


“Kumekuwepo na wimbi kubwa la mmonyonyoko wa maadili kupitia njia mbalimbali hasa kupitia uchapaji wa picha chafu katika mitandao na wasanii wengi wa muziki na filamu wamekuwa ni miongoni mwa kundi linaloongoza kwa upigaji picha za kudhalilisha na kutumiwa na mitandao mbalimbali, na kwa kuwa hili suala ni mtambuka serikali inashirikiana na TCRA ili kudhibiti hali hii isiendelee”alikaririwa . 


Akitoa ufafanuzi kuhusu hatua zinazochukuliwa na Serikali, Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia, Prof. Makame Mbarawa, amesema serikali itachukua hatua dhidi ya wote watakaobainika kusambaza picha zinazokiuka maadili, zikiwemo zinazowaonyesha watumishi wa umma.



Tafiti zinaonyesha kuwa, teknolojia inatajwa kuwa moja ya kichocheo kikubwa cha kubadili mienendo ya binadamu bila kujali misingi ya kimaadili, ambapo mabadiliko hayo yanatajwa kujikita zaidi katika matumizi ya mitandao ya kijamii ikiwemo ‘facebook’, ‘Instagram’, ‘Twitter’ na ’Whatsapp’ ambayo vijana wengi wamekuwa wakitumia muda mwingi kuwasiliana na watu wa aina mbalimbali na baadae kuvuja kwa sababu mbalimbali.

0 Responses to “SERIKALI YATANGAZA KUKOMAA NA WANAOPIGA PICHA CHAFU NA KUZIWEKA KWENYE MITANDAO”

Post a Comment

More to Read