Friday, July 25, 2014

VIWANDA VITATU KUTOZWA FAINI YA MILIONI 90 KWA KUVURUGA MAZINGIRA.


VIWANDA vitatu vinakabiliwa na adhabu ya faini ya Sh milioni 90 kutokana na kushindwa kutimiza masharti ya kuhifadhi mazingira katika uendeshaji wake.

Hayo yalisemwa na Mwanasheria wa Baraza la Taifa la Hifadhi ya Mazingira (NEMC), Manchare Heche wakati wa majumuisho ya ziara ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais, Dk Binilith Mahenge kutembelea baadhi ya viwanda jijini hapa.

Alisema viwanda vitakavyodhibitiwa ni kiwanda cha M.M Integrated Steel Mills Ltd, Bidco Oil & Soap Limited, na kiwanda cha Murzah Oil Mills Limited na kwamba kila kimoja kitatozwa faini ya Sh milioni 30.

Katika ziara hiyo Dk Mahenge alibaini kuwa kiwanda cha Murzah hakina mashine ya kutibu majitaka yanayozalishwa na kiwanda hicho na hivyo kusababisha maji hayo kuathiri mazingira na afya za wananchi.

“Hali hii haikubaliki hata kidogo, hivyo lazima mtumie mashine zinazotakiwa kutibu majitaka, na tunasema hivi si kwa kiwanda chako tu, hivyo tunataka hili litekelezwe,” alisema Dk Mahenge alimweleza meneja wa kiwanda hicho Dinesh Kana baada ya kushuhudia majitaka ya kiwanda hicho.

Kutokana na hali hiyo, kiwanda hicho kilipewa mwezi mmoja kufunga mashine hiyo na kupewa wiki mbili kukutana na viwanda vilivyoko barabara ya Nyerere na wadau wengine kutatua changamoto ya maji na miundombinu.

Kiwanda cha Bidco kilipewa miezi sita kuhakikisha kinabadili chanzo cha nishati baada ya kubainika kutumia magogo ya miti kama chanzo kikuu cha nishati, hali ambayo inachangia kuharibu mazingira.

Akizunguzia suala hilo, Ofisa Mazingira Manispaa ya Ilala, Abdon Mapunda alimwonesha Waziri Mahenge mtaro unaodaiwa kupitisha majitaka kutoka viwanda vilivyoko kwenye barabara ya Nyerere kuingiza kwenye bwawa la majitaka la Vingunguti.

0 Responses to “ VIWANDA VITATU KUTOZWA FAINI YA MILIONI 90 KWA KUVURUGA MAZINGIRA.”

Post a Comment

More to Read