Thursday, November 13, 2014
KONDOMU ZAZUA KIZAAZA NCHINI TANZANIA.
Do you like this story?
Imeelezwa
kuwa maambukizi ya Virusi vya Ukimwi (VVU), yanaweza kuongezeka nchini hasa kwa
vijana kutokana na kubainika kupungua kwa kasi ya matumizi ya mipira (kondomu).
Hayo yalielezwa jana na Katibu Mkuu,
Ofisi ya Waziri Mkuu, Dk Florens Turuka katika mkutano wa sita wa kutathmini
maambukizi ya VVU nchini.
Dk
Turuka amesema maambukizi mapya yameendelea kuwapo kwa sababu vijana hawatumii
kondomu kujikinga.
“Matumizi
ya kondomu katika jamii yamepungua na kuwafanya watu wengi hasa vijana kupata
maambukizi na zaidi ni kutokana na mwamko mdogo kuhusu umuhimu wa kondomu kama
kinga ya Ukimwi,” amesema.
Alisema
utafiti uliofanyika mwaka jana ulionyesha kuwa asilimia 50 ya waliojitokeza
kupima VVU na kupata ushauri, walikiri kutotumia kondomu. Hata hivyo, Dk Turuka
alisema katika kipindi cha miaka 10 iliyopita, maambukizi mapya yalipungua
kutoka watu 180,000 hadi 72,000 kwa mwaka.
Amesema
licha ya kuwapo mafanikio hayo, kiwango cha matumizi ya kondomu kimeshuka na
kuhatarisha maisha ya vijana wenye umri kati ya miaka 15 – 39.
Amesema
mwaka ujao wa fedha, Serikali itaanzisha mfuko maalumu wa kukusanya fedha kwa
ajili ya kununulia dawa za kupunguza makali ya ugonjwa huo (ARV).
Amesema
zaidi ya nusu ya wagonjwa walioathirika wanahitaji dawa hizo.
Mwenyekiti
Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Kudhibiti Ukimwi (Tacaids), Fatma Mrisho alisema
wanafanya jitihada kuhakikisha wanapunguza maambukizi mapya hadi kufikia sifuri
ifikapo mwaka 2020.
Aliitaja
baadhi ya mikoa yenye idadi kubwa ya maambukizi mapya kuwa ni Njombe,
Shinyanga, Mbeya, Dar es Salaam na Ruvuma.
“Katika miaka miwili
ijayo, tutaelekeza nguvu zetu kwenye mambo yanayochangia kuongezeka kwa
maambukizi mapya, ikiwamo maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto na
kukabiliana na uhaba wa dawa,” amesema.
Na Peter Elias, Mwananchi
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “KONDOMU ZAZUA KIZAAZA NCHINI TANZANIA.”
Post a Comment