Wednesday, January 27, 2016

STIKA MAALUM ZENYE UJUMBE WA KUPINGA MAUAJI YA WATU WENYE ALBINISM ZAZINDULIWA DAR


Kamanda Siro ambaye alikuwa mgeni rasmi katika tukio hilo, akikata utepe rasmi kwa ajili ya uzinduzi huo.

Baadhi ya washiriki wakifuatilia mkutano huo wakiwemo watu hao wenye albinism hapa nchini.

Makamanda mbalimbali wa jeshi la Polisi wakishuhudia tukio hilo..

Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar Es Salaam, Simon Sirro akiwa ameshikilia ‘stika’ maalum yenye ujumbe wa kupinga mauaji na ukatili dhidi ya watu wenye albinism nchini. Kamanda Siro amezindua stika hizo jana jijini Dar es Salaam huku zikitarajiwa kufika katika mikoa yote ya Tanzania.  Wanaoshuhudia ni waratibu wa stika hizo kutoka chama cha Albino Enterprises Dar es Salaam na wageni wao. (Picha na Andrew Chale, modewjiblog).


Taasisi ya watu wenye ulemavu wa ngozi (Albino) ‘Enterprises of Dar es Salaam-AED’ kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, mapema jana  26 Januari, imezindua stika maalumu yenye ujumbe wa kutokomeza mauaji ya watu hao wenye Albinism.

Stika hiyo imebeba ujumbe wa “Ewe ndugu Mtanzania tuungane na Mh. Rais Dk. John Pombe Magufuli, Jeshi la Polisi na wadau mbalimbali katika kutokomeza mauaji ya ndugu zetu wenye albinism. Kwa pamoja tunaweza.”
Uzinduzi wa stika hiyo unalenga kuhamasisha jamii kuwapenda, kuwafariji na kuwahakikishia usalama wao albino pia kuwa huru kifikra kwa kujilinganisha na watu wasio na ulemavu wa ngozi.

Akisoma risala iliyoandaliwa na taasisi ya AED mtunza fedha wa taasisi hiyo Mwamvua Kambi kwa mgeni rasmi Kamanda wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Kamanda Simon Siro amesema kuwa, kutokomeza mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi ni kazi ngumu inayohitaji ushirikishwaji wa kila mtu.

Mwamvua amesema kuwa watu wenye ulemavu wa ngozi nchini wanakabiliwa na mauaji ya aina tatu ambayo ni mauaji ya kisaikolojia yanayomgusa kila albino hasa kwa kushuhudia vitendo vya kikatili vya ukataji viungo vya wenye ualibino vilipoibuka.

Pia, mauaji yanayosababishwa na saratani ya ngozi ambayo hutokana na ukosefu wa mafuta ya ngozi yanayo kinga athari za mionzi ya jua na vikingia jua. Vilevile mauaji ya kukatwa viungo ambayo jamii inayatambua hadi sasa.

Mkurugenzi wa taasisi hiyo Michael Lugendo amesema mikakati itakayotumiwa kufikia lengo la kutokomeza mauaji hayo ni pamoja na kusambaza stika kwa njia ya nyumba za ibada, kutumia mawakala nchi nzima, kutumia vituo vya kudumu katika maeneo yenye watu wengi.

Pamoja na kutumia ligi ndogo za mpira wa miguu kama ligi iliyoanzishwa inayoitwa Balozi Samata Cup ambayo lengo lake ni kuibua vipaji, kutoa elimu kuhusu masuala ya albinism na kusambaza stika. Ligi hiyo itaanza tarehe 30 Januri mwaka huu.

“Tuna mpango wa kuteua mabalozi wengine kutoka makundi mbalimbali ili kushirikiana na Mbwana Samata kuleta matokeo chanya katika kubadilisha historia ya wenye ulemavu wa ngozi Tanzania,” amesema Lugendo.

Akizindua stika Kamanda Simon Siro amesema kuwa, ni wajibu wa kila mtu kwa nafasi yake kuhakikisha albino wanaishi kwa amani na usalama pia aliwahakikishia kuwa jeshi la polisi litatoa ushirikiano katika kudhibiti mauaji hayo.

“Kuna baadhi ya maeneo bado ya dhana potofu ya kuamini kuwa kupata kiungo cha albino ni kuwa tajiri, huu si ukweli sababu tatizo la ualbino ni la kibaiolojia. Mikoa ya kanda ya ziwa inaongoza kwa kuwa na kesi nyingi za mauaji ya kikatili ya albino. Inabidi mikoa hiyo ipewe elimu ya kutosha,” 

amesema Siro na kuongeza:
“Vyombo vya dola vinawajibika kupata taarifa za matukio hayo na kuwafanyia kazi watuhumiwa kwa kuwachukulia hatua kali za kisheria ili kutokomeza tatizo hili.”
Siro amewataka wananchi na wenyeviti wa serikali za mitaa kujua idadi ya albino waishio kwenye maeneo yao, kuwahakikishia ulinzi pamoja na kutoa taarifa wanapopata matatizo na kutoa taarifa mapema kama kuna watu wenye nia mbaya nao ili kuzuia matukio hayo.

Viongozi wa dini wametakiwa kutoa elimu ya kiroho kwa waumini wao juu ya athari za mauaji ya kikatili ya albino na kutoa msaada kwa albino waliokumbwa na janga hili la ukatwaji wa viungo vyao.

Taasisi imewaomba wadau mbalimbali kama wasanii, wanasiasa, viongozi wa taasisi za kidini na wafanyabiashara kutoa msaada watakaopo hitaji msaada wao wa hali na mali.

0 Responses to “ STIKA MAALUM ZENYE UJUMBE WA KUPINGA MAUAJI YA WATU WENYE ALBINISM ZAZINDULIWA DAR”

Post a Comment

More to Read