Wednesday, January 27, 2016
STIKA MAALUM ZENYE UJUMBE WA KUPINGA MAUAJI YA WATU WENYE ALBINISM ZAZINDULIWA DAR
Do you like this story?
Kamanda Siro ambaye alikuwa mgeni rasmi katika tukio hilo, akikata utepe rasmi kwa ajili ya uzinduzi huo. |
Baadhi ya washiriki wakifuatilia mkutano huo wakiwemo watu hao wenye albinism hapa nchini. |
Makamanda mbalimbali wa jeshi la Polisi wakishuhudia tukio hilo.. |
Taasisi ya watu wenye ulemavu wa ngozi (Albino) ‘Enterprises of Dar es
Salaam-AED’ kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam,
mapema jana 26 Januari, imezindua stika maalumu yenye ujumbe wa
kutokomeza mauaji ya watu hao wenye Albinism.
Stika hiyo imebeba ujumbe wa “Ewe ndugu Mtanzania tuungane na Mh. Rais
Dk. John Pombe Magufuli, Jeshi la Polisi na wadau mbalimbali katika kutokomeza
mauaji ya ndugu zetu wenye albinism. Kwa pamoja tunaweza.”
Uzinduzi wa stika hiyo unalenga kuhamasisha jamii kuwapenda, kuwafariji
na kuwahakikishia usalama wao albino pia kuwa huru kifikra kwa kujilinganisha
na watu wasio na ulemavu wa ngozi.
Akisoma risala iliyoandaliwa na taasisi ya AED mtunza fedha wa taasisi
hiyo Mwamvua Kambi kwa mgeni rasmi Kamanda wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam,
Kamanda Simon Siro amesema kuwa, kutokomeza mauaji ya watu wenye ulemavu wa
ngozi ni kazi ngumu inayohitaji ushirikishwaji wa kila mtu.
Mwamvua amesema kuwa watu wenye ulemavu wa ngozi nchini wanakabiliwa na
mauaji ya aina tatu ambayo ni mauaji ya kisaikolojia yanayomgusa kila albino
hasa kwa kushuhudia vitendo vya kikatili vya ukataji viungo vya wenye ualibino
vilipoibuka.
Pia, mauaji yanayosababishwa na saratani ya ngozi ambayo hutokana na
ukosefu wa mafuta ya ngozi yanayo kinga athari za mionzi ya jua na vikingia
jua. Vilevile mauaji ya kukatwa viungo ambayo jamii inayatambua hadi sasa.
Mkurugenzi wa taasisi hiyo Michael Lugendo amesema mikakati itakayotumiwa
kufikia lengo la kutokomeza mauaji hayo ni pamoja na kusambaza stika kwa njia
ya nyumba za ibada, kutumia mawakala nchi nzima, kutumia vituo vya kudumu
katika maeneo yenye watu wengi.
Pamoja na kutumia ligi ndogo za mpira wa miguu kama ligi iliyoanzishwa
inayoitwa Balozi Samata Cup ambayo lengo lake ni kuibua vipaji, kutoa elimu
kuhusu masuala ya albinism na kusambaza stika. Ligi hiyo itaanza tarehe 30
Januri mwaka huu.
“Tuna mpango wa kuteua mabalozi wengine kutoka makundi mbalimbali ili
kushirikiana na Mbwana Samata kuleta matokeo chanya katika kubadilisha historia
ya wenye ulemavu wa ngozi Tanzania,” amesema Lugendo.
Akizindua stika Kamanda Simon Siro amesema kuwa, ni wajibu wa kila mtu
kwa nafasi yake kuhakikisha albino wanaishi kwa amani na usalama pia
aliwahakikishia kuwa jeshi la polisi litatoa ushirikiano katika kudhibiti
mauaji hayo.
“Kuna baadhi ya maeneo bado ya dhana potofu ya kuamini kuwa kupata kiungo
cha albino ni kuwa tajiri, huu si ukweli sababu tatizo la ualbino ni la
kibaiolojia. Mikoa ya kanda ya ziwa inaongoza kwa kuwa na kesi nyingi za mauaji
ya kikatili ya albino. Inabidi mikoa hiyo ipewe elimu ya kutosha,”
amesema Siro
na kuongeza:
“Vyombo vya dola vinawajibika kupata taarifa za matukio hayo na kuwafanyia
kazi watuhumiwa kwa kuwachukulia hatua kali za kisheria ili kutokomeza tatizo
hili.”
Siro amewataka wananchi na wenyeviti wa serikali za mitaa kujua idadi ya
albino waishio kwenye maeneo yao, kuwahakikishia ulinzi pamoja na kutoa taarifa
wanapopata matatizo na kutoa taarifa mapema kama kuna watu wenye nia mbaya nao
ili kuzuia matukio hayo.
Viongozi wa dini wametakiwa kutoa elimu ya kiroho kwa waumini wao juu ya
athari za mauaji ya kikatili ya albino na kutoa msaada kwa albino waliokumbwa
na janga hili la ukatwaji wa viungo vyao.
Taasisi imewaomba wadau mbalimbali kama wasanii, wanasiasa, viongozi wa
taasisi za kidini na wafanyabiashara kutoa msaada watakaopo hitaji msaada wao
wa hali na mali.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “ STIKA MAALUM ZENYE UJUMBE WA KUPINGA MAUAJI YA WATU WENYE ALBINISM ZAZINDULIWA DAR”
Post a Comment