Thursday, February 25, 2016

WANAFUNZI 575 SINGIDA WATUMIA MATUNDU MANNE YA VYOO.




Wanafunzi 575 wa shule ya msingi Ipuli, Tarafa ya Nduguti, Wilayani Mkalama, Mkoani Singida wanatumia matundu ya vyoo manne kati ya matundu 31 yanayohitajika katika shule hiyo, jambo ambalo linasababisha baadhi yao kwenda kujisaidia mashamabani huku wengine wakijisaidiaa kwenye vyoo vya muda vilivyozungushiwa maturubai.

Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Ipuli, Jeremia Masawe aliyasema hayo kwenye taarifa aliyotoa kwa Mbunge wa jimbo la Iramba mashariki (CCM), Allani Joseph Kiula aliyetembelea shuleni hapo kutaka kufahamu changamoto zinazoikabili shule hiyo.

Aidha mwalimu huyo alifafanua kwamba kabla ya kuamua kujenga matundu hayo sita ya vyoo kulikuwa na matundu mengine waliyokuwa wakiyatumia wanafunzi lakini kutokana na kuta zake kuwa na nyufa walilazimika kusitisha matumizi ya vyoo hivyo.

Hata hivyo mwalimu Masawe aliweka wazi kuwa baada ya mvua kubwa iliyonyesha Disemba, 17 mwaka jana ndipo matundu hayo yote yalipopitiwa na hivyo waliamua kusitisha matumizi yake na kuanza ujenzi wa matundu mengine ya vyoo vya kudumu.

“Shule ilikuwa na choo chenye matundu manne lakini kutokana na mvua zilizokuwa zinaendelea kunyesha ndipo mnamo tarehe 17/12/2015 matundu yote hayo manne yalipopitiwa hivyo tukaanza ujenzi mwingine lakini wakati huu tukatengeneza utaratibu mwingine wa vyoo vya muda wanafunzi wataendelea kuvitumia wakati tunaandaa vyoo vya kudumu.” alisisitiza mwalimu mkuu huyo.

Kwa mujibu wa mwalimu huyo wanafunzi 575 waliopo katika shule hiyo wanahitaji jumla ya matundu 31 ya vyoo na kwamba hata hayo wanayoendelea kujenga hayatatosheleza mahitaji ya wanafunzi hao.

“Vyoo vilivyokuwa vikitumika kwa siku za nyuma vikawa vimeachwa kwa sababu ya kuta zake kuwa na nyufa kwa hivyo tukaondoa zile kuta tukafunga maturubai kwa ajili ya wanafunzi kujisaidia huku wengine wakijificha mashambani,” alisisitiza mwalimu mkuu huyo.

Kwa upande wake mbunge wa jimbo la Iramba Mashariki(CCM), Allani Joseph Kiula ambaye alitembelea shule hiyo na kushiriki katika ujenzi wa matundu hayo ya vyoo alisema kuwa mikakati ya Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama ni kuhakikisha shule zote zinakuwa na matundu ya vyoo vya kudumu.

“Kimsingi ni kwamba mimi kama mbunge, madiwani na Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama tunao mkakati wa kuhakikisha kwamba shule zote zinapata matundu ya kutosha ya vyoo na tunataka ifanyike hivyo kwa sababu sasa hivi kuna ugonjwa wa kipindupindu kwa hiyo tanataka tuhakikishe kwamba suala la vyoo mashuleni linamalizika kabisa,” alisema Kiulla

Hata hivyo mbunge Kiula aliweka bayana kwamba mpaka sasa wameshafanya sensa na kupata takwimu za kubaini mahitaji ya shule zenye upungufu wa matundu ya vyoo kwa hivyo nguvu zaidi zitaelekezwa katika ujenzi wa matundu ya vyoo vya kutosha.
Imeandaliwa na Jumbe Ismailly, Singida.

0 Responses to “ WANAFUNZI 575 SINGIDA WATUMIA MATUNDU MANNE YA VYOO.”

Post a Comment

More to Read