Thursday, February 25, 2016
WANAFUNZI 575 SINGIDA WATUMIA MATUNDU MANNE YA VYOO.
Do you like this story?
Wanafunzi 575 wa shule ya msingi Ipuli, Tarafa ya Nduguti, Wilayani
Mkalama, Mkoani Singida wanatumia matundu ya vyoo manne kati ya matundu 31
yanayohitajika katika shule hiyo, jambo ambalo linasababisha baadhi yao kwenda
kujisaidia mashamabani huku wengine wakijisaidiaa kwenye vyoo vya muda
vilivyozungushiwa maturubai.
Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Ipuli, Jeremia Masawe aliyasema hayo
kwenye taarifa aliyotoa kwa Mbunge wa jimbo la Iramba mashariki (CCM), Allani
Joseph Kiula aliyetembelea shuleni hapo kutaka kufahamu changamoto
zinazoikabili shule hiyo.
Aidha mwalimu huyo alifafanua kwamba kabla ya kuamua kujenga matundu hayo
sita ya vyoo kulikuwa na matundu mengine waliyokuwa wakiyatumia wanafunzi
lakini kutokana na kuta zake kuwa na nyufa walilazimika kusitisha matumizi ya
vyoo hivyo.
Hata hivyo mwalimu Masawe aliweka wazi kuwa baada ya mvua kubwa
iliyonyesha Disemba, 17 mwaka jana ndipo matundu hayo yote yalipopitiwa na
hivyo waliamua kusitisha matumizi yake na kuanza ujenzi wa matundu mengine ya
vyoo vya kudumu.
“Shule ilikuwa na choo chenye matundu manne lakini kutokana na mvua
zilizokuwa zinaendelea kunyesha ndipo mnamo tarehe 17/12/2015 matundu yote hayo
manne yalipopitiwa hivyo tukaanza ujenzi mwingine lakini wakati huu
tukatengeneza utaratibu mwingine wa vyoo vya muda wanafunzi wataendelea
kuvitumia wakati tunaandaa vyoo vya kudumu.” alisisitiza mwalimu mkuu huyo.
Kwa mujibu wa mwalimu huyo wanafunzi 575 waliopo katika shule hiyo
wanahitaji jumla ya matundu 31 ya vyoo na kwamba hata hayo wanayoendelea
kujenga hayatatosheleza mahitaji ya wanafunzi hao.
“Vyoo vilivyokuwa vikitumika kwa siku za nyuma vikawa vimeachwa kwa
sababu ya kuta zake kuwa na nyufa kwa hivyo tukaondoa zile kuta tukafunga maturubai
kwa ajili ya wanafunzi kujisaidia huku wengine wakijificha mashambani,”
alisisitiza mwalimu mkuu huyo.
Kwa upande wake mbunge wa jimbo la Iramba Mashariki(CCM), Allani Joseph
Kiula ambaye alitembelea shule hiyo na kushiriki katika ujenzi wa matundu hayo
ya vyoo alisema kuwa mikakati ya Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama ni
kuhakikisha shule zote zinakuwa na matundu ya vyoo vya kudumu.
“Kimsingi ni kwamba mimi kama mbunge, madiwani na Halmashauri ya Wilaya
ya Mkalama tunao mkakati wa kuhakikisha kwamba shule zote zinapata matundu ya
kutosha ya vyoo na tunataka ifanyike hivyo kwa sababu sasa hivi kuna ugonjwa wa
kipindupindu kwa hiyo tanataka tuhakikishe kwamba suala la vyoo mashuleni
linamalizika kabisa,” alisema Kiulla
Hata hivyo mbunge Kiula aliweka bayana kwamba mpaka sasa wameshafanya
sensa na kupata takwimu za kubaini mahitaji ya shule zenye upungufu wa matundu
ya vyoo kwa hivyo nguvu zaidi zitaelekezwa katika ujenzi wa matundu ya vyoo vya
kutosha.
Imeandaliwa na Jumbe Ismailly, Singida.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “ WANAFUNZI 575 SINGIDA WATUMIA MATUNDU MANNE YA VYOO.”
Post a Comment