Monday, December 5, 2016
MIKOA SITA YARIPOTIWA KUWA NA KIPINDUPINDU,TAYARI WATU SITA WAMEPOTEZA MAISHA
Do you like this story?
Baada ya maambukizi ya ugonjwa wa kipindupindu kusimama
kwa zaidi ya miezi mitatu, ugonjwa huo umelipuka tena katika mikoa sita
Tanzania Bara na kusababisha vifo sita, huku idadi ya wagonjwa iliyoripotiwa
kuanzia mwezi Oktoba ikiongezeka kutoka 250 hadi 458 Novemba mwaka huu.
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na
Watoto, Ummy Mwalimu wakati akitoa ripoti ya ugonjwa huo kwa wanahabari,
amesema Mkoa wa Morogoro unaongoza kwa idadi ya wagonjwa kwa kuwa na wagonjwa
282, ukifuatiwa na Dodoma 96, Mara 31, Kigoma 30, Arusha 11 na Dar es Salaam ikiwa
na wagonjwa 8.
“Kipindupindu bado tunacho nchini licha ya kusimama
kwa miezi mitatu hadi minne. Mwezi Oktoba mikoa 4 iliripotiwa kuwa na ugonjwa
huo, Novemba imeongezeka na kufikia mikoa 6. Oktoba wilaya zilizokuwa na
wagonjwa zilikuwa 6, Novemba zikawa 14. Kwa upande wa wilaya Kilosa inaongoza
kwa kuwa na wagonjwa 236 ikifuatiwa na Mpwapwa yenye wagonjwa 88,” amesema.
Ummy ametaja sababu ya ugonjwa huo kulipuka tena kuwa
ni ukosefu wa vyoo bora na maji safi na salama, utiririshaji maji mata, pamoja
na baadhi ya Halmashauri kuficha taarifa za wagonjwa wapya.
Kufuatia sababu hizo, Ummy ameagiza ifikapo Juni 5,
2017 kila kaya nchini iwe na choo bora na kwamba kaya isiyotekeleza agizo hilo
itachukuliwa hatua.
“Asilimia 34 ya kaya nchini ndizo zenye vyoo bora,
natoa miezi 6 kila kaya iwe na choo bora. Halmashauri kuanzia sasa zianze
kufanya ukaguzi ili kubaini kaya zisizokuwa na choo bora,” amesema.
Pia, ameagiza kila halmashauri nchini kutoficha
taarifa za ugonjwa wa kipindupindu kwa kuhofia watendaji wake kusimamishwa
kazi.
“Halmashauri nyingi zinaficha taarifa za wagonjwa wa
kipindupindu kwa kuhofia kutumbuliwa, matokeo yake wagonjwa wa kipindupindu
wanachanganywa na wagonjwa wengine, huu ni uuaji, tunatoa tahadhari kwa
wahusika watoe taarifa mapema ili ugonjwa huu udhibitiwe,” amesema.
Ameziagiza halmashauri ambazo kata zake hazina kamati
ya afya kuanzisha kamati hizo ili ziweze kusimamia usafi na kufuatilia mwenendo
wa ugonjwa wa kipindupindu.
Aidha, Ummy amesema serikali itawachukulia hatua
maafisa afya wa kata watakaoshindwa kudhibiti utitirishaji maji taka katika
mitaa.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “ MIKOA SITA YARIPOTIWA KUWA NA KIPINDUPINDU,TAYARI WATU SITA WAMEPOTEZA MAISHA”
Post a Comment