Monday, December 5, 2016

WAZIRI JAFFO ATOA SIKU 4 KWA MIKOA YOTE NCHINI




MIKOA yote Tanzania Bara imepewa siku nne kuhakikisha inatoa idadi ya vituo vya afya vitakavyoingizwa kwenye mfumo wa ukusanyaji wa mapato ya Serikali za Mitaa kwa njia ya kielektroniki.

Agizo hilo limetolewa leo na Suleiman Jaffo, Naibu Waziri wa Nchi, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na kwamba, mpaka sasa sasa vituo 65 pekee kati ya 5511 ndivyo vilivyofungiwa mfumo huo.

Jaffo amesema hayo wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya kuwajengea uwezo timu ya wawezeshaji wa kitaifa wa mfumo wa ukusanyaji mapato wa serikali za mitaa kwa njia ya kielektronik GoT-HoMIS na LGRCIS.

Mafunzo hayo yameandaliwa na wataalamu kutoka Shirika la Elimu Kibaha na Chuo Kikuu Mzumbe wakishirikia Kurugenzi ya Uimarishaji Mifuko ya Sekta za Umma (PS3) kwa ufadhili wa Shirika la Misaada la Marekani (USAID) yaliyofanyika Chuo Kikuu Mzumbe mkoani humo.

Amesema serikali ilifanya uamuzi wa kuwa na mfumo mmoja wa kielektroniki wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ulioandaliwa na wataalamu hao utakaotumika katika kusimamia, kuboresha na kuimarisha utoaji wa huduma bora za afya.

Lakini pia ukisaidia ukusanyaji mapato hasa katika menejimenti ya upokeaji na utoaji wa madawa na vifaa tiba na shughuli zingine za sekta ya afya kama ilivyo kwenye mfumo wa mapato wa LGRCIS.

Amesema mikoa mingi haijafanya vizuri katika kutoa idadi ya vituo vya afya na hivyo kujikuta kila mkoa ukiwa chini ya asilimia 10 jambo linaloleta maana tofauti katika mikoa husika kwenye suala nyeti kama hilo.

“Hatuwezi kwenda kama tunafanya mambo kwa mazoea na haiwezekani mkoa ukaleta idadi ya vituo chini ya vituo 10 katika mkoa, hapo sitawaelewa,” amesema Jaffo.

Jaffo amewataka viongozi kuwa wasimamizi wazuri katika matumizi ya mifumo hiyo ya kielektronik kufuatia tabia iliyojionesha awali ya uwepo wa baadhi ya vituo kutumia njia ya kielektronik kwa muda mfupi na baadaye kuacha na kuhamia kwenye vitabu kwa maslahi yao binafsi.

Amesema kwamba, ukusanyaji wa mapato hayo kwa njia ya kielektronik una lengo zuri la kuboresha makusanyo kufuatia mikoa iliyojaribiwa kuonesha mafanikio.

Ametolea mfano Mkoa wa Mwanza katika kituo cha Kololeni ambapo awali makusanyo yalikuwa ni Sh. 4.8 Mil na sasa ni Sh. 6 Mil.

0 Responses to “WAZIRI JAFFO ATOA SIKU 4 KWA MIKOA YOTE NCHINI”

Post a Comment

More to Read