Sunday, March 23, 2014
YANGA ,MBEYA CITY VITANI.
Do you like this story?
Mabingwa watetezi Yanga baada ya kutoka sare
mara mbili mfululizo leo watashuka kwenye Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi
kuwakabili Rhino Rangers kwa lengo moja tu la kusaka ushindi ili kuendelea
kuipa presha Azam FC kileleni wa Ligi Kuu Bara.
Azam inaongoza ligi kwa tofauti ya pointi nne
kwa Yanga ingawa vijana hao wa Jangwani wanajivunia kuwa na akiba ya mchezo
mmoja mkononi, hivyo watataka kushinda ili kuipiga kumbo Azam kileleni.
Tangu walipotolewa katika Ligi ya Mabingwa na
Al Ahly, Yanga wametoka suluhu 0-0 na Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Jamhuri,
kabla ya kutoka sare 1-1 na Azam Jumatano iliyopita kwenye Uwanja wa Taifa, Dar
es Salaam.
Wakongwe hao wa soka la Tanzania, wapo katika
nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi wakiwa na pointi 40, wakati
Azam inakalia kiti cha uongozi ikiwa na pointi 44.
Wapinzani wao Rhino kwa sasa wanakamata mkia
ikiwa pointi 13 baada ya kucheza mechi 20 na kuonja ushindi mechi 2, sare saba
na kupigwa mara 11.
Endapo Yanga itafanikiwa kuizamisha Rhino
itafikisha pointi 43 ambazo zitapunguza pengo kati yake na Azam yenye
pointi 44, pia itaepuka hatari ya kushushwa chini ya Mbeya City iliyoko nafasi
ya tatu ikiwa na pointi 38 na ambayo leo itaumana na JKT Ruvu kwenye Uwanja wa
Azam Complex.
Kocha wa Yanga, Hans van der Pluijm amesema
matokeo ya sare ya bao 1- 1 waliyoyapata dhidi ya Azam yameharibu mipango
yao lakini amewataka wachezaji wake kusahau yote na kuhakikisha wanashinda kila
mechi iliyo mbele yao wakianzia na Rhino Rangers.
Yanga imebakiwa na mechi saba dhidi
ya Rhino, Prisons, Kagera Sugar, Mgambo, JKT Ruvu, Oljoro JKT na Simba
wakati Azam imebakiwa na mechi dhidi ya Oljoro JKT, Mgambo JKT, Simba,
Ruvu Shooting, Mbeya City na JKT Ruvu.
Pluijm amesema kuwa walikuwa na kila
sababu ya kuibuka na ushindi katika mechi yao ya juzi Jumatano dhidi ya Azam
kwani walipata nafasi nyingi za kufunga lakini bado jinamizi la kukosa
mabao linazidi kuwaandama washambuliaji wake.
Kocha huyo wa Uholanzi anaamini kama
wangeshinda mchezo huo wangejiwekea mazingira mazuri zaidi ya kutwaa
ubingwa lakini sare hiyo imewarudisha nyuma na sasa ni kama wanaanza upya
mapambano.
“Hatupaswi kukata tamaa na matokeo hayo
ingawa tulistahili kushinda kwani tulitengeneza nafasi nyingi
hatukuzitumia, kipindi cha kwanza tulicheza vizuri sana, lakini kipindi
cha pili tulipoa jambo ambalo lilitugharimu.
“Sasa hivi kubwa ni kucheza kwa malengo na
kuhakikisha tunashinda mechi zote tulizobakiwa nazo huku tukiombea mpinzani
wetu apoteze mechi mbili tu, nawaamini vijana wangu hawataniangusha, ingawa si
jambo rahisi kwani tuna mechi tatu za ugenini hivyo inabidi tufanye kazi
kubwa,” alisema Pluijm.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “YANGA ,MBEYA CITY VITANI.”
Post a Comment