Wednesday, October 15, 2014
MKUU WA MKOA AKATAA KIINGEREZA KUTUMIKA KWENYE WARSHA, KISA WAJUMBE HAWAIELEWI HIYO LUGHA
Do you like this story?
MKUU wa Mkoa wa Singida, Dk Parseko Kone juzi alilmtaka mshereheshaji
katika warsha ya wadau wa rasimu ya mpango wa usimamizi na uendelezaji wa
pamoja wa rasilimali za maji Bonde la Kati kuacha kuendesha utambulisho wa
wajumbe hao kwa lugha ya Kiingereza badala yake atumie Kiswahili.
Alilazimika kuingilia kati baada ya kushuhudia baadhi ya wajumbe
waliokuwa wakitambulishwa na kutakiwa kusimama ili waonekane kushindwa kufanya
hivyo kwa kile kilichodhihirika wazi kupigwa na bumbuwazi na utambulisho huo wa
lugha ya Kiingereza.
Akionesha wazi kukerwa kwake na mshehereshaji, Dk Kone alisema wakati
taifa liko katika juhudi za kukuza Kiswahili, baadhi ya Watanzania wanakwamisha
juhudi hizo kwa sababu hafifu kama za kuwepo baadhi ya washiriki wasiojua
Kiswahili.
“Wajumbe wa warsha hii wako 200 na wasioelewa Kiswahili ni wanne tu.
Idadi hii ndogo haiwezi kusababisha mkutano huu uendeshwe kwa Kiingereza. Wengi
wetu hapa japo tunajua Kiingereza, baadhi yetu mwaka umepita bila kukizungumza;
hivyo inahitaji mtu kujiandaa ili kuwa katika nafasi nzuri ya kukizungumza,”
alisema.
Aidha, alisema endapo warsha hiyo ingeendeshwa kwa lugha ya Kiingereza,
wachangiaji wa rasimu hiyo wangekuwa wachache hivyo kuwanyima wengi fursa ya
kutoa mawazo yao.
Katika hotuba yake ya ufunguzi, Mkuu huyo wa Mkoa aliwataka wadau
kushirikiana katika kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazokabili usimamizi
wa rasilimali za maji kutokana na suala hilo kuwa mtambuka.
Alizitaja baadhi ya changamoto hizo kuwa ni migogoro inayohusu maji
pamoja na siasa.
Alisema Sekta ya Maji ina jukumu kubwa katika maendeleo ya kijamii na
kiuchumi, lakini kwa bahati mbaya inakabiliwa na changamoto mbalimbali ambazo
bila kutatuliwa huathiri utekelezaji wa mipango na mikakati ya maendeleo na
usimamizi wa rasilimali za maji.
Bonde la Kati lenye makao yake makuu mkoani Singida ni miongoni mwa
mabonde tisa yaliyopo nchini na linajumuisha maeneo ya Dodoma, Manyara,
Singida, Tabora, Shinyanga, Arusha na Kilimanjaro ambapo linagusa jumla ya
wilaya 26. Ni la pili kwa ukubwa likiwa na kilomita za mraba 143,099.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “MKUU WA MKOA AKATAA KIINGEREZA KUTUMIKA KWENYE WARSHA, KISA WAJUMBE HAWAIELEWI HIYO LUGHA ”
Post a Comment