Wednesday, October 8, 2014

FFU NJOMBE WATUMIA MAMBOMU YA MACHOZI KUTULIZA VURUGU ZA WANAFUNZI SHULE YA SEKONDARI NJOSS ,WANAFUNZI WACHOMA MOTO BWENI


Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani Njombe, Fulgence Ngonyani akiangalia bweni la wanafunzi wa shule ya sekondari Njombe ambalo limeteketea kwa moto usiku wa kuamkia leo.
Askari akimwangalia mmoja wa wanafunzi ambaye anapelekwa kupakizwa kwenye gari kwa ajili ya kwenda kituo cha polisi kwa mahojiano zaidi.

Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani Njombe, Fulgence Ngonyani akitazama gari dogo ambalo ni la mwalimu Benard Nyamahonga lililovunjwavunjwa vioo vyake na wanafunzi hao.



Askari wa Jeshi la Polisi mkoani Njombe wakiwa wamewaweka chini ya ulinzi baadhi ya wanafunzi wa shule ya sekondari Njombe (Njosi) wakati wakisubiri kupelekwa kituo cha polisi leo.


ASKARI  wa kutuliza  ghasia (FFU) mkoa wa Njombe leo walazimika  kutumia mabomu ya machozi kuwatawanya wanafunzi wa  shule ya sekondari Njombe (NJOSS )baada ya vurugu   kubwa  kuibuka jana katika  shuleni hapo  kwa wananfunzi wa shule  hiyo  ya wavulana  kuteketeza kwa  moto  bweni la shule  hiyo  pamoja na kuharibu  majengo ya  shule ya Msingi Kilimani kwa mawe .

Kutokana na  vurugu  hizo  shule  hiyo  imefungwa kwa muda wa  mwezi mmoja kuanzia sasa  ili  kupisha ukarabati mkubwa wa majengo ya  shule  hiyo .


Afisa Elimu wa Mkoa wa Njombe, Said Nyasiro  alitoa agizo la kufungwa kwa  shule hiyo kwa mwezi huo  mmoja  hadi  Novemba 8  huku wanafunzi hao wakitakiwa kurejea shuleni hapo na kiasi cha shilingi 150,000 kila mmoja kama fidia ya mali  zilizoharibiwa

Katika tukio hilo, askari polisi walilazimika kutumia mabomu ya machozi kuwatawanya wanafunzi waliokuwa wakifanya vurugu, wanaosoma Kidato cha Tano na Sita, ambao walifanya uharibifu wa kuchoma moto eneo la shule linalozunguka lenye miti na kuharibu pia gari dogo Toyota Carina namba: T809 BBX la Mwalimu wa Nidhamu, Benard Nyamahonga kwa kulivunjavunja vioo kwa mawe.

Kama hiyo haitoshi, wanafunzi hao walikwenda katika nyumba ya mwalimu mkuu wa shule hiyo, Benard William na kurusha mawe yaliyovunja vioo vya madirisha ya nyumba hiyo.

Kufuatia tukio hilo, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Njombe, Fulgence Ngonyani pamoja na maofisa wa Upelelezi kutoka jeshi hilo alithibitisha kutokea tukio hilo na kufanya ukaguzi wa kutembelea maeneo yaliyoharibiwa, sambamba na kupata taarifa za awali kutoka kwa walimu wa shule hiyo.

Kamanda Ngonyani ambaye alikataa kuzungumzia kwa undani juu ya tukio hilo, ambapo alisema bado wanachukua maelezo, alisema taarifa rasmi ya juu ya upelelezi wa tukio hilo itatolewa.

Hata hivyo askari wa Jeshi la Polisi, walikuwa wamezunguka katika eneo lote la shule ya Sekondari Njombe kwa ajili ya kuweka ulinzi kuhakikisha hakuna wanafunzi yeyote anayetoroka kwa ajili ya hofu ya kukamatwa.

Askari hao ambao walikuwa wamevaa dhana zao za kudhibiti fujo wakiwemo askari wa kikosi cha kutuliza ghasia (FFU) pamoja na askari wa upelelezi, katika hatua ya awali ya kuwabaini wanafunzi waliofanya uharibifu huo, waliitisha paredi ya wanafunzi wote na kufanya uhakiki wa kubaini waliohusika na tukio hilo.

Katika zoezi hilo la utambuzi, zaidi ya wanafunzi zaidi ya 40 walitambulika awali kuwa vinara wa vurugu hizo, ambapo walipandishwa kwenye magari mawili ya polisi kupelekwa kituo kikuu cha polisi kwa ajili ya mahojiano zaidi.

Akizungumzia kuhusu tukio hilo lilivyotokea, Isabela Malangalila, Ofisa Mtendaji wa Mtaa wa Mpechi na Joshoni ambako ndiko shule hiyo ilipo, alisema vurugu za wanafunzi kuanza kuchoma moto mabweni hayo zilianza mnamo saa 5 usiku jana.

“Kabla ya tukio hilo, jana kulikuwa na kikao cha Wazazi na Walimu wa shule ya sekondari Mpechi ambacho kilikuwa kinawahoji wanafunzi 29 waliokuwa wamekwenda kwenye disko katika chuo cha Maendeleo ya Jamii bila ya kupata ruhusa,” alisema  Malangalila.

Alisema katika kikao hicho, wanafunzi waliobainika kwenda kwenye disko hilo akiwemo pia mwanafunzi mmoja aliyekutwa na simu ya mkononi waliambiwa waandike maelezo, lakini jambo la kushanga baadaye jana usiku wanafunzi zaidi ya 1000 wanaosoma shule hiyo waliandamana na kuanzisha vurugu huku wakirusha mawe hovyo na kutishia kuchoma moto shule hiyo.

“Kufuatia vitisho hivyo niliwasiliana na kikosi cha zima moto kufika haraka kwenye eneo la shule, na hapo ndipo moto ulipoanza kuwaka kwenye bweni namba nane, baadhi ya wanafunzi walijitahidi kuzima moto uliokuwa ukiwaka katika bweni hilo,” alisema Malangalila.

Mtendaji huyo wa Mtaa alisema pia, wanafunzi hao waliendelea kufanya uharibifu zaidi kwa kuvunja duka la shule, kung’oa mboga zilizopandwa kwenye bustani, kisha kuwasha moto eneo la shule na kwenda kuharibu gari dogo la mwalimu wa nidhamu ambalo walilivunjavunja kwa mawe vioo vyake pamoja nakuvunja vioo vya nyumba ya mwalimu huyo.

“Hali hii inatisha na kusikitisha, wanafunzi hao walipofanya huo uharibifu walikwenda pia katika shule ya Msingi Kilimani na kuvunja madarasa pamoja na kuchanachana madaftari ya wanafunzi wa shule hiyo ambao wako darasa la pili, huku wakiwa wameandika maandishi ukutani yakisema ‘Sisi wanafunzi wa Njosi tumekuja kulala tu’,” alisema Malangalila.

Naye Mkuu wa shule hiyo, Mwalimu Benard William akizungumzia tukio hilo, alisema bweni ambalo limeathirika sana kwenye tukio hilo ni lile la namba nane ambalo linauwezo wa kuchukua wanafunzi 102.

Aidha mwalimu William alisema kwamba chanzo cha wanafunzi hao kufanya vurugu hizo zinatokana na madai yao kwamba wamechoshwa kunyanyaswa ikiwemo kuonewa kwa wanafunzi wenzao 30 ambao walisimamishwa masomo.

“Huu ni utukutu usiositahili kuvumiliwa, unakatisha tamaa sana kwetu sisi walimu, madai yao ambayo wanayalalamikia kimsingi hayajitoshelezi, kwani walipotoroka kwenda kucheza disko katika chuo cha maendeleo ya jamii mmoja wao alivunjika mguu na hadi sasa anatembelea magongo,” alisema William.

Mwenyekiti wa Bodi ya shule hiyo, Maria Mdee akizungumzia tukio hilo alisema haamini kilichofanywa na wanafunzi hao, na kuliita tukio hilo kuwa ni miongoni mwa matukio mabaya yaliyogusa sana maisha yake.

“Inasikitisha sana hasa ikizingatiwa kwamba wanafunzi ambao walikuwa wakiwahoji jana walikuwa bado hawajafukuzwa shule, bali wasimamishwa tu masomo mpaka hapo watakapo waleta wazazi wao, na Oktoba 7 tulikutana na wazazi na wanafunzi hao kwa ajili ya kuwaeleza makosa yao,” alisema Mdete.

Alisema kufuatia tukio hilo zima, athari itakuwa kubwa hivi sasa katika shule hiyo kwa baadhi ya wanafunzi ambao hawakuhusika na tukio hilo, kwani mwezi Novemba walikuwa wanatarajia kufanya mtihani wa mkoa kabla ya kufanya mtihani wa Taifa.

Mwenyekiti huyo alisema kufuatia tukio hilo, uongozi wa shule hiyo utasubili tamko la Afisa Elimu wa mkoa wa Njombe kama shule hiyo itafungwa ili wanafunzi warejee majumbani hadi hapo baadaye.

Afisa Elimu wa mkoa wa Nkombe, Said Nyasiro akiwa na Ofisa Elimu wa shule za Sekondari mkoani hapa, Venance Msungu walifika katika eneo la shule hiyo na kutembelea kuangaria uharibifu uliotokea na kufanya mkutano wa ndani na walimu wa shule hiyo ambao ulichukua zaidi ya saa mbili, ambapo waandishi wa habari hawakuruhusiwa kuingia.

Kamanda wa Polisi, Ngonyani akiwa na maofisa wake, pamoja na walimu na viongozi hao wa wizara ya Elimu walifanya mkutano wa ndani, lakini alipotoka kwenye mkutano huo aliwaambia waandishi wa habari kuwa tukio hilo atalizungumzia mara baada ya kufanya tathimini ili kubaini thamani ya mali zilizotekea.

Hili ni tukio la pili  sasa kutokea kwa shule hiyo ya sekondari Njombe, ambapo mwaka mmoja uliopita, wanafunzi wa shule hiyo walichoma moto bweni ambalo hivi sasa lipo kwenye ujenzi.
*Mwandishiwetu Michael Katona matukiodaima.co.tz Njombe*

0 Responses to “ FFU NJOMBE WATUMIA MAMBOMU YA MACHOZI KUTULIZA VURUGU ZA WANAFUNZI SHULE YA SEKONDARI NJOSS ,WANAFUNZI WACHOMA MOTO BWENI”

Post a Comment

More to Read