Thursday, March 3, 2016
KAMPUNI ZA SIMUNCHINI ZAPIGWA FAINI YA MAMILIONI.
Do you like this story?
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Dkt. Ally Simba. |
MAMLAKA ya Mawasiliano Tanzania (TCRA)
imetoza kampuni tano za simu za mkononi, faini ya Sh milioni 112.5 kutokana na
kushindwa kutekeleza masharti na vigezo vya ubora wa huduma.
Ingawa haikuelezwa moja kwa moja vigezo vya
ubora wa huduma walivyokiuka, TCRA imezungumzia malalamiko ya wateja ya kukatwa
fedha na kampuni bila kupiga simu, na kukiri kukithiri kwa tatizo hilo. Ilisema
wanatarajia kufunga mtambo utakaokuwa ukifuatilia bando katika simu za wateja,
kukabili tatizo husika.
Kampuni zilizoadhibiwa kwa kukiuka Kanuni ya
Ubora wa Huduma za Sheria ya Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta za mwaka
2011, ni Airtel Tanzania Limited, Benson Informatics Limited (Smart), MIC
Tanzania Limited (Tigo), Vodacom Tanzania Limited na Zanzibar Telecom Limited
(Zantel).
Akizungumza jana na waandishi wa habari,
Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Dk Ally Simba alisema TCRA imebaini kampuni hizo
hazitoi huduma bora. Ilibaini hilo baada ya kutathmini ubora wa huduma za
mawasiliano (Sauti na data) zinazotolewa na kampuni hizo. Tathmini ililenga
kupata uhalisia wanaoupata watumiaji wa huduma hizo.
“Kwa kuzingatia makampuni hayo kukubali
kutotimiza vigezo vya ubora wa huduma wanazotoa na kuahidi kuboresha, Mamlaka
imetoa adhabu kwa mujibu wa kanuni za ubora wa huduma kama ilivyoainishwa
katika Kanuni 15 ya Kanuni ya Ubora wa Huduma,” alisema.
Alitaja kampuni na faini (kwa shilingi)
wanazotakiwa kulipa ndani ya mwezi mmoja ni Airtel (Sh milioni 22.5), Benson
Informatics Limited(Sh milioni 12.5), Tigo (Sh milioni 25), Vodacom (Sh milioni
27.5) na Zantel (Shmilioni 25).
“Endapo makampuni hayo yatashindwa kutoa
faini hizo katika muda waliotakiwa kutoa au makosa hayo kujirudia rudia,
watachukuliwa hatua kali zaidi, ikiwa ni pamoja na kufutiwa leseni,” alisema.
Dk Simba aliwasisitiza watoa huduma za simu
za mikononi, kuhakikisha huduma hizo zinazingatia vigezo vilivyoainishwa
kupitia Kanuni za Ubora wa Huduma na kuboresha huduma hizo katika kipindi cha
miezi sita. Alisema mamlaka itaendelea kufanya uchunguzi wa ubora wa huduma za simu
sehemu mbalimbali nchini, kila baada ya miezi mitatu.
CHANZO: HABARI LEO
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “ KAMPUNI ZA SIMUNCHINI ZAPIGWA FAINI YA MAMILIONI.”
Post a Comment