Wednesday, March 9, 2016

TRA YAFUTA KODI ELEKEZI KWA WAFANYABIASHARA


Kaimu Kamishna wa TRA, Alphayo Kidata akifafanua jambo waandishi wa habari (Hawapo pichani) kuhusu mpango wa Serikali kuwasaidia wananchi wa kipato cha chini ili waweze kumudu kulipa kodi


Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imefuta kodi elekezi kwa bidhaa zinazoingizwa nchini kwa msamaha wa kodi hususani zile zinazotoka nchini China kwa kuwata wafanyabiashara wanaoagiza na kuingizi bidhaa kutoka huko kulipa kodi inayotakiwa.

Hayo yamesemwa leo na Kaimu Kamishna wa TRA, Alphayo Kidata alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika utaratuibu wa kuongea na umma kwa kuwapa taarifa kuhusu makusanyo ya kodi ya kila mwezi.
 
Kaimu Kamishna  huyo amesema kuwa Serikali kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania imeamua kufuta kodi elekezi ambayo ilikuwa inawapa punguzo la kodi wafanyabiashara wanaoagiza na kuingiza bidhaa toka nchini China kwa kupunguziwa sehemu ya kodi.

“Tumeamua kuondoa kodi elekezi kwasababu haina faida kwa taifa letu kwani inawanyima wafanyabiashara wengine ambao hawaagizi bidhaa kutoka China fursa ya kushindana kibiashara na Serikali yetu sio ya kibaguzi ndio maana tumaeamua kufuta kodi hii  ili kuleta usawa kwa wafanyabiashara wote nchini”Alisema Kidata.

“Suala liliopo kwa sasa ni kwa kila mwananchi anayepaswa kulipa kodi katika kitu anachokifanya alipe kodi na atutafumbia macho ukwepaji wa kodi na hakuna kitu kinachoitwa kodi elekezi wala msamaha wa kodi katika Serikali hii, tulipe kodi kwa maendeleo ya taifa letu” aliongeza Kidata.

Aidha, Kamisha Kidata amesema kuwa hakuna Sheria yoyote inayosema kuwa kutakuwa na kodi elekezi ama msamaha wa kodi kwa mfanyabiashara yoyote yule bali ule  ulikuwa ni utaratibu tu uliowekwa na Mamlaka na baada ya  kuona hauna umuhimu wala faida katika nchini yetu ikaamriwa ufutwe.

Katika kusisitizi suala la kufutwa kodi elekezi na utekelezaji wake Kaimu Kamishna wa kodi za Ndani toka TRA, Salum Yusuf amesema watalisimamia suala la ulipaji kodi na yeyote atakayekaidi kulipa kodi kwa Mamlaka husika watawachukulia hatua za kisheria na kusisitiza kuwa kulipa kodi ni jukumu la kila mtanzania katika kuleta maendeleo ya taifa letu.

Mamlaka ya Mapato Tanzania imekuwa na rekodi nzuri ya ukusanyaji wa kodi tangu mwezi Desemba mwaka 2015 kwa kukusanya zaidi ya shillingi trillioni 1 na wanaendelea na kasi ya kukusanya kodi zaidi na kwa takwimu zilizopo kuanzia mwezi Julai mwaka 2015 mpaka mwezi Februari mwaka huu wamekusanya jumla ya shillingi trillioni 8.6 ikiwa ni asilimia 99 ya malengo waliojiwekea.

0 Responses to “ TRA YAFUTA KODI ELEKEZI KWA WAFANYABIASHARA”

Post a Comment

More to Read