Tuesday, November 8, 2016
BURIANI BABU: NIMJUAVYO SAMWEL JOHN SITTA
Do you like this story?
Alfajiri ya
leo, Novemba 7, 2016 imekuwa siku ya huzuni na majonzi makubwa kwa Taifa.
Tuliamka na kukutana na habari za kusikitisha juu ya kifo cha Mzee wetu Samwel
John Sitta, Spika Mstaafu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mzee
Sitta alikuwa mgonjwa kwa kitambo kidogo, lakini bado tulikuwa na matumaini
kuwa afya yake ingetengamaa na kuendelea kuwa nasi.
Habari hizi
za kufariki dunia kwake zilizosambaa kwa kasi kubwa kupitia mitandao ya kijamii
zimetushtusha mno. Hatimaye taarifa rasmi ikatoka kuthibitisha habari hizo.
Kuwa Mzee watu amefariki dunia akiwa kwenye matibabu nchini Ujerumani.
Samwel John
Sitta aliitumikia nchi yetu kwa muda mrefu na kwa uadilifu mkubwa sana. Si
hivyo tu, sisi wengine pia kwa kiasi flani Hata kukua kwetu kisiasa kumetokana
na utumishi wake uliotukuka kwa nchi yetu alipokuwa Spika wa Bunge la Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania. Katika tanzia hii ninamkumbuka Mzee Sitta Kwa namna
nilivyofungamana naye binafsi na namna nilivyomshuhudia katika kazi zake
mbalimbali za uongozi.
Samwel Sitta
ananigusa mimi binafsi moja kwa moja. Alikuwa Babu yangu. Tukiwa Bungeni
akiniandikia kitu alikuwa akitumia neno hilo 'babu' kwa mwandiko wake mzuri
usiotoka kwenye kumbukumbu zangu kabisa. Labda siku za usoni 'vinote' (vimemo)
hivi vinaweza kuchapishwa pindi watafiti watakapokuwa wakiandika historia ya
nchi yetu na Bunge letu. Hivyo siku zote za maisha yetu nilimuita babu.
Disemba 29,
2005 mzee Sitta aliniapisha kiapo cha ubunge tarehe. Maneno ambayo aliniambia
baada ya kunikabidhi Kanuni za Bunge na Katiba ya Nchi niliyaandika kwenye
daftari langu la kumbukumbu siku hiyo hiyo jioni. Baada ya kula kiapo cha Utii
na cha uaminifu kawaida Wabunge hupewa mkono na mwapishaji na kupewa nyaraka za
kazi.
Kwangu
haikuwa hivyo, Mzee Sitta alinikumbatia na kuniambia "Utakuwa Kiongozi
muhimu sana kwa nchi yetu. You have a bright future (unayo kesho njema)".
Maneno haya hayajawahi kunitoka katika kumbukumbu zangu, ni maneno ya faraja na
msukumo wa kunitaka kwenda mbele kila ninapopata misukosuko ya kisiasa. Mara
kadhaa yeye mwenyewe alikuwa akinipigia na kunikumbusha juu ya maneno yake haya
na kunitia moyo.
Babu Sitta
alikuwa Mlezi wa wanasiasa vijana, binafsi amenilea na kunisomesha. Mwaka 1996
nilikuwa mwanafunzi wa Kidato cha Tano (Form Five) katika Shule ya Sekondari ya
Galanos ya jijini Tanga, nikisomea mchepuo wa Historia, Jiografia na Uchumi
(HGE). Hali ya hewa ya jiji la Tanga haikunipenda, hivyo nikawa naumwa mara kwa
mara. Lakini pia sikupenda kusoma HGE, nilitaka kusoma Hisabati badala ya
Historia. Wakati wa likizo ya mwezi Disemba mwaka 1996, nilitoka Tanga nikaenda
Dar es Salaam, Wizara ya Elimu kuomba uhamisho kwenda shule yenye Somo la
Hisabati kidato cha Tano na Sita. Nikakataliwa. Lakini nikaambiwa kuwa
Mkurugenzi wa Elimu ya Sekondari wakati ule, ndugu Ndeki alisoma pamoja na
Samwel Sitta.
Kipindi hicho
Mzee Sitta akiwa Mkurugenzi wa Investments Promotion Centre (IPC) mara kabla
haijabadilishwa jina kuwa Tanzania Investments Centre (TIC) mara baada ya kuwa
mbunge wa Urambo kwa miaka 20 (1975 - 1995). Nikaenda Ofisi za IPC, zilizokuwa
mahala ambapo leo ni Benki ya CRDB Tawi la Azikiwe. Nilipofika Katibu Muhtasi
wake akaniuliza kama nina miadi na bosi wake, nikasema hapana. Akaniambia
hawezi kukuona. Nikasisitiza sana na kumlilia dada yule aniruhusu hata kwa
akika chache tu. Akaniruhusu.
Nilipofika
Mzee Sitta aliniuliza shida zangu kwa heshima kubwa. Nikamwambia kwamba ninataka
kuhama shule. Akaniomba matokeo yangu ya Kidato cha Nne, nikampa maana nilikuwa
natembea nayo. Alipoyasoma akaniambia, "wewe hupaswi kuhangaika kutafuta
shule maana kwa matokeo yako unaweza kusoma shule yeyote nchini ya chaguo
lako". Akainua simu akampigia ndugu Ndeki kumuomba anihamishe.
Kisha
akaniandikia kikaratasi niende Wizarani muda ule ule. Nilipofika Wizarani
nikapewa uhamisho kwenda Shule ya Sekondari Mazengo. Nilipotoka nje ya Wizara
nikakutana na kijana mwengine, Godfrey Hiluka, anaomba uhamisho, yeye anatoka
Mazengo anataka kwenda Tosamaganga Iringa. Akaniambia, achana na Mazengo hakuna
Mwalimu wa Uchumi na hali ya vyoo ni mbaya sana.
Nikarudi kwa
Mkurugenzi. Mtumishi aliyenijazia fomu za Uhamisho (Mzee wa Makamo) aliponiona
narudi na kumwambia sitaki kwenda Mazengo, akachukua fomu zangu za uhamisho na
akachukua 'kifuta - wino' (whiteout) akafuta Mazengo na kuweka Tosamaganga huku
akisema kwa hasira "nyie watoto wa wakubwa bwana!"Sikujali nikaenda
zangu Tosamaganga kusoma Uchumi, Jiografia na Hisabati (EGM).
Samwel John
Sitta akaendelea kufuatilia maendeleo yangu shuleni, mpaka Chuo Kikuu cha Dar
es Salaam na baadaye Taasisi ya InWent nchini Ujerumani. Nilipotoka Ujerumani
kusoma masomo ya Juu ya Biashara ya Kimataifa mwaka 2004 nilipaswa niwe na
mradi wa kitaaluma. Nikachagua kuunganisha makampuni ya Kijerumani na makampuni
ya Tanzania kwa kuandika mradi wa kuchukua wafanyabishiara 20 kutoka Tanzania
na kuwaunganisha na wengine 20 kutoka nchi za Jumuiya ya Ulaya.
Ilibidi
kupata Taasisi ya Tanzania kwa ajili mradi huo na Mzee Sitta akawa mstari mbele
kuhakikisha Mradi unafanikiwa na tukautekeleza kwa umakini kwa msaada wa afisa
wa TIC aitwaye Phina Lyimo. Mafungamano yetu hayakuishia hapo, mwaka mmoja
baadaye tukakutana na Mzee Sitta Bungeni, yeye akiwa Mbunge wa Jimbo la Urambo
Mashariki na mimi nikiwa Mbunge wa Jimbo la Kigoma Kaskazini. Ulezi wake kwangu
ukaendelea mpaka mauti yalipomkuta leo mapema asubuhi. Taifa limepoteza
Kiongozi mzalendo, lakini mimi nimepoteza pia 'babu Mlezi'.
Samwel John
Sitta alikuwa Mwanamageuzi (Reformer), na kupitia uanamageuzi wake alifanya
mabadiliko makubwa sana katika uendeshaji wa shughuli za Bunge akiwa Spika wa
Bunge kwa miaka mitano. Sisi tuliohudumu kwenye Bunge la tisa chini yake,
tukimwita Spika wa Viwango na Kasi, tuliona wenyewe juhudi zake za kuliweka
Bunge katika nafasi yake ya Kikatiba.
Licha ya
kuhakikisha kuwa maslahi ya Wabunge yanakuwa yanayolingana na hadhi ya Bunge,
alihakikisha pia kuwa Bunge linaisimamia Serikali sawa sawa. Haikuwa kazi
rahisi sana kwani kulikuwa na mvutano mkubwa sana kati ya Spika Sitta na Waziri
Mkuu Edward Lowasa katika kuleta mabadiliko hayo.
Tulikuwa
tunaambiwa kuwa mvutano ule ulitokana na tetesi kwamba Sitta ndiye alipaswa
kuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na hivyo kuwa na msuguano
na aliyeteuliwa kushika nafasi hiyo badala yake. Sio Sitta wala Lowasa ambaye
alithibitisha ama kukanusha tetesi zile. Sitta ametangulia mbele ya haki, labda
Edward Lowasa ataweza kusemea hili siku za usoni.
Samwel Sitta
alitumia fursa ya msuguano huo kufanya mabadiliko makubwa ya kanuni za Bunge na
kutoa uhuru mpana wa mawazo ndani ya Bunge na kuhakikisha kuwa Taarifa za
Kamati za Bunge, hususan Kamati za Usimamizi wa Serikali, zinakuwa zinasomwa na
kujadiliwa ndani ya Bunge kwa mujibu wa Kanuni.
Wakati wa
Bunge la 8 chini ya mzee Pius Msekwa, Taarifa za CAG hazikuwahi kusomwa hata
mara moja bungeni. Ni kutokana na mabadiliko haya ya kanuni ndipo Kamati ya
Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC ) ilianzishwa mwezi Machi, mwaka
2008. Nilichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa kwanza wa Kamati ile na kuingia kwenye
Kamati ya Uongozi ya Bunge ambayo kipindi hicho tuliiona kama Kamati ya Wabunge
wazee.
Namna
nilivyoingia kuwa Mwenyekiti wa POAC nayo ni hadithi nyengine ya namna ya
malezi ya kiuongozi yalifanywa na Spika Sitta. Sikuwa nimejaza fomu kuomba hata
ujumbe wa Kamati ya POAC. Wakati huo ulikuwa ni wakati wa vuguvugu la Buzwagi
(Mkataba wa Madini uliosainiwa na Waziri wa Nishati Hotelini nchini Uingereza
kwa siri).
Nilikuwa
mjini Bagamoyo kwenye kazi za Kamati ya Bomani (Kamati iliyoundwa na Rais
kuchunguza mikataba na sheria za madini) nikiwa na Harrison Mwakyembe na
Ezekiel Maige. Spika wa Bunge akanipigia simu, akaniambia "Babu, kesho
kuna uchaguzi wa Kamati za Bunge. Nimekuteua Kamati ya POAC ambayo ni Kamati
mpya itakayokuwa chini ya Kambi ya Upinzani. Najua hukuomba kuwa mjumbe wa
Kamati hii, lakini nahitaji damu changa kwenye Kamati ya Uongozi ya Bunge.
Naomba unikubalie na kesho uwepo Dar es Salaam kwa ajili ya uchaguzi na
ugombee. Utashinda maana nimeshafanya kazi yangu".
Sikuwa na
namna ya kukataa japo nilitaka sana kuendelea kuwa mjumbe wa Kamati ya Fedha na
Uchumi chini ya marehemu Abdallah Kigoda, ama Kamati ya Nishati na Madini chini
ya Mzee William Shelukindo. Lakini ombi la Mzee ni amri. Nikawa Mwenyekiti wa
POAC na kuwa mmoja wa washauri wakuu wa Spika wa Bunge. Kamati ya PAC ikawa
chini ya Mzee John Momose Cheyo na Kamati ya LAAC ikawa chini ya Dkt. Willibrod
Peter Slaa. Ilikuwa ni Bunge lenye meno kweli kweli.
Spika Sitta
alikuwa mbabe. Ubabe wake ulimpelekea kufanya maamuzi ambayo wakati mwengine
yalimweka kwenye matatizo na wananchi. Mfano mzuri ni masuala ya 'Hoja Binafsi
ya Buzwagi' na 'Hoja ya Wizi wa Fedha Benki Kuu (EPA)'. Mwanzoni, Spika alikuwa
upande wa Wabunge wenye hoja hizo, yaani mimi na Dkt. Wilbroad Slaa kiasi cha
kuziboresha hoja zile kwa kalamu yake mwenyewe. Wabunge wa chama chake hawakuwa
wanapenda hoja hizi na hivyo Waziri Mkuu Edward Lowasa akamweka kwenye wakati
mgumu sana wa kuegemea upande wa Serikali.
Hoja ya dkt
Slaa akaitupa kuwa 'Ni makaratasi ya kuokoteza'. Hoja yangu akaiingiza Bungeni
na akasimamia kusimamishwa kwangu Bungeni baada ya kuwasilisha hoja hiyo.
Wananchi walimkasirikia sana. Siku moja usiku, nikiwa nyumbani kwa ndugu
Freeman Mbowe Mikocheni, Spika Sitta akanipigia simu kulalamika kuwa wafuasi
wangu wanamtukana kwa ujumbe wa simu (sms), akanitaka niwakataze. Nilimkubalia
tu, lakini sikuwa na uwezo huo. Nchi ilikuwa imevimba. Ilikuwa Oktoba 2007.
Samwel Sitta alijua namna ya kuisoma nchi, na akamua kuwapa wananchi watakacho,
wakati mwengine.
Mwezi
Novemba, katika kujibu kiu ya wananchi kuhusu uwajibikaji na kufuta makosa ya
Buzwagi na EPA, Spika alisimamia kuundwa kwa Kamati Teule kuchunguza suala la
Mkataba wa Richmond. Yaliyofuata yalikuwa historia. Taarifa ya Kamati Teule
husika ilipelekea kuanguka kwa Serikali kwa mara ya kwanza katika hsitoria ya Tanzania.
Waziri Mkuu Edward Lowasa alilazimika kujiuzulu ndani ya Bunge, Baraza la
Mawaziri likavunjika na Serikali mpya kuundwa chini ya Waziri Mkuu mpya, ndugu
Mizengo Pinda. Spika Samwel Sitta akawa ni Spika wa pili wa nchi yetu
aliyeshuhudia uundwaji wa Serikali mbili ndani ya miaka mitano ya uspika wake.
Mzee Msekwa
yeye alikaa kwenye Uspika kwa miaka 13. Miaka 10 na Waziri Mkuu mmoja, ndugu
Sumaye. Akianzia Uspika Mwaka 1993. Mwaka mmoja mbele akishuhudia mabadiliko ya
Mawaziri Wakuu, kutoka mzee John Malecela kwenda kwa mzee Cleopa Msuya. Baada
ya kujiuzulu kwa Lowasa, Samwel Sitta hakurudi nyuma tena. Aliendelea kuwa
Spika wa Viwango mpaka alipomaliza muda wake katika Bunge la Tisa.
Sifa nyengine
ya Spika Sitta ni Uungwana, alikuwa mwepesi mno wa kuomba msamaha pale
alipokosea. Nakumbuka siku moja mwaka 2009 alimfukuza Bungeni Mzee mwenzake
John Cheyo kwa makosa ambayo Mzee Cheyo hakufanya. Baadhi yetu tukakasirishwa
sana na kitendo kile. Nikaenda kumwona Mzee Sitta ofisini kumwuliza kulikoni
amdhalilishe mwenzake namna ile. Akanieleza kuwa hakuwa sawa na atamwomba radhi
John Cheyo. Tukiwa kwenye Kamati ya Uongozi ya Bunge, kwa ajenda zake za
kawaida tu, Mzee Sitta akamwomba radhi Mzee Cheyo.
Nikikumbuka
kisa hiki hutabasamu, maana Jaji Werema, aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali
alicheka mpaka kuanguka chini. Sababu? Mzee Sitta aliketi kwenye kiti chake,
wenyeviti wote wa Kamati tukiwa tumetulia tuanze kikao. Mzee Sitta akasema
"John, naomba radhi kwa tukio lililotokea Bungeni wiki iliyopita. Sijui
nilikuwa nina nini siku hiyo?, nadhani nilisumbuliwa na watu wanaopitapita
jimboni kutaka kunitoa, nisamehe Mzee mwenzangu".
Kicheko
ukumbi mzima na mzee John Cheyo akamkubalia radhi yake huku naye akicheka na
yakaishia hapo. Wazee hawa wawili wameandika pamoja Kitabu "Bunge lenye
Meno".
Nimwelezeje
zaidi Babu? Nimwelezeje zaidi Spika wa Kasi na Viwango Samwel John Sitta?
Mwanasiasa Shupavu, Jasiri, Mwenye Ngozi Ngumu, Mbabe, Mnyenyekevu inapobidi na
mwenye Uthubutu. Tangulia Babu. Tangulia Mjukuu wa Fundikira. Tangulia Mtemi wa
Unyanyembe Samwel John Sitta. Ingawa umeondoka duniani, bado unaishi kupitia
kazi zako za Kizalendo kwa Nchi yetu.
Kabwe Z.
Ruyagwa Zitto
Novemba 7,
2016
Dodoma
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “BURIANI BABU: NIMJUAVYO SAMWEL JOHN SITTA”
Post a Comment