Monday, March 17, 2014
MAKACHERO WAPEKUA NYUMBANI KWA RUBANI, MALAYSIA.
Do you like this story?
Kuala Lumper. Polisi nchini Malaysia
wamevamia nyumba aliyokuwa akiishi rubani wa ndege iliyopotea na kuendesha
msako mkali, ikiwamo kukusanya nyaraka muhimu ambazo zinazamiwa kuwa zitasaidia
kufichua ukweli kuhusu tukio la kupotea kwa ndege hiyo.
Ripoti zimesema kuwa upekuzi huo, ambao pia
umefanyika katika nyumba aliyokuwa akiishi rubani msaidizi, umefanyika baada ya
kuibuka kwa taarifa zinazodai kuwa rubani huyo, Zaharie Ahmad Shah alikuwa na
mrengo wa siasa kali.
Shah alikuwa ni shabiki na mfuasi wa wazi wa
mwanasiasa wa upinzani, Anwar Ibrahim ambaye sasa yupo gerezani baada ya
kukutwa na hatia ya kujihusisha na vitendo vya fedheha.
Inaaminika kuwa rubani huyo alikuwapo
mahakamani wakati mwanasiasa huyo alipopandishwa kizimbani mwezi Machi mwaka
huu na pengine hakufurahishwa na hukumu hiyo.
Kwa sasa polisi wanashikilia nyaraka kadhaa,
ikiwamo kompyuta ambayo inadhaniwa kuwa na taarifa muhimu zilizohifadhiwa na
rubani huyo.
Polisi hao wameenda mbali zaidi kwa kuanzisha
uchunguzi wa kimazingira ambao utasaidia kupata historia binafsi kuhusu maisha
ya rubani huyo aliyetajwa kuwa na uzoefu mkubwa wa urushaji wa ndege.
Wataalamu wa saikolojia na wale wanaohusika
na usalama wa anga wameitwa kuongeza nguvu ili kusaidia kuchambua taarifa
zinazoendelea kukusanywa kuhusu mwenendo wa rubani Shah ambaye nyumba yake bado
inaendelea kulindwa.
Kitendo cha polisi kuifanyia upekuzi nyumba
ya rubani huyo pamoja na kukusanya taarifa zake binafsi kimeelezwa kwamba ni
jitihada za Serikali kutaka kujiridhisha hasa kutokana na mazingira
yanayohusisha upotevu wa ndege hiyo.
Wachunguzi hao wanataka kujua kama kumekuwa
na tukio lolote la matatizo ya kiakili na kumewahi kujitokeza kwa changamoto za
kifamilia kwa marubani hao au kwa yeyote aliyekuwamo kwenye ndege hiyo
iliyokuwa ikisafiri kutoka Kuala Lumpur na kuelekea Beijing.
Pamoja na kwamba marubani wa ndege hiyo ya
Malaysia walikuwa na rekodi nzuri, kuna wasiwasi pengine walikutwa na tukio
lililosababisha kujiingiza kwenye hali ambayo ingepoteza umakini wa kuongoza
ndege.
Uchunguzi pia unawalenga abiria waliokuwemo
kwenye ndege hiyo iliyokuwa na umri wa miaka 11 na kwamba hatua hiyo inaweza
kusaidia upatikanaji ukweli halisi juu ya tukio hilo.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “MAKACHERO WAPEKUA NYUMBANI KWA RUBANI, MALAYSIA.”
Post a Comment