Friday, March 28, 2014
MCHAKATO KUMNGO”A SPIKA EALA WAANZA.
Do you like this story?
Wabunge wa Bunge la Afrika Mashariki (Eala) wameanza
rasmi mchakato wa kumwondoa madarakani spika wao, Margareth Zziwa kutoka Uganda
baada ya kuwasilisha hati ya kusudio hilo kwa katibu wa bunge hilo, Kenneth
Madete.
Habari zilizotufikia na kuthibitishwa na
katibu wa Bunge la Eala, Keneth Madete zinaeleza kuwa hati hiyo inayotoa fursa
kwa hoja hiyo kuwasilishwa rasmi bungeni, iliwasilishwa juzi asubuhi.
“Huenda hoja hiyo ikajadiliwa Jumanne ijayo,”
alisema Madete baada ya kuthibitisha kuwa ofisi yake imepokea barua hiyo.
Baadhi ya wabunge waliozungumza kwa sharti la
kutotajwa majina yao, walisema barua hiyo imewasilishwa baada ya kufuata
taratibu zote ikiwa ni pamoja na kusainiwa na wabunge wanne kutoka kila nchi.
“Kikanuni tumewasilisha kusudio la hoja ya
kutokuwa na imani na spika kwa muda usiopungua Saa 24, kabla ya hoja hiyo
kuwasilishwa rasmi na tayari tumetekeleza hilo leo (juzi), asubuhi,” alisema
mmoja wa wabunge hao.
Kwa mujibu wa kanuni, hati hiyo inatakiwa kusainiwa
na wabunge wasiopungua wanne kutoka kila nchi mwanachama; EAC inaundwa na nchi
tano za Tanzania, Uganda, Kenya, Burundi na Rwanda, ambapo kila nchi
huwakilishwa na wabunge tisa na hivyo kufanya idadi yao kuwa 45.
Mwenyekiti wa wabunge wa Tanzania, Adam
Kimbisa alisema hadi sasa yeye binafsi na kwa nafasi yake kama kiongozi wa
wenzake hajapata taarifa rasmi kuhusu kusudio hilo wala ombi la kusaini hati ya
kumng’oa spika.
Ofisa habari na mawasiliano ya Umma wa Eala,
Bobi Odiko alisema hadi jana bado hakuwa amepata taarifa rasmi ya mkakati huo
ingawa alikiri kuzisikia. Katibu wa bunge hilo, Kenneth Madete hakupatikana
jana kuzungumzia suala hili baada ya kutokupatikana ofisini kwake wala kwa njia
ya simu.
Pamoja na mambo mengine, wabunge wa Eala
wanapanga kumng’oa spika wao kwa madai ya kushindwa kumudu majukumu yake,
upendeleo kwenye safari za nje miongoni mwa wabunge, ambapo baadhi
wanajirudia katika ziara huku wengine wakiambulia safari chache.
Zziwa, ambaye ni mwanamke wa kwanza kushika
wadhifa huo ndani ya EAC, pia anatuhumiwa kupachika ndugu zake kwenye timu ya
Bunge la Uganda na kulipwa posho wakati wa michezo ya kibunge iliyofanyika
jijini Kampala mwishoni mwa mwaka jana.
Spika wa kwanza wa Eala alikuwa Abdulrahama
Kinana wa Tanzania, aliyefuatiwa na Abdirahim Abdi kutoka Kenya aliyepokewa na
Ziwa.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “MCHAKATO KUMNGO”A SPIKA EALA WAANZA.”
Post a Comment