Friday, March 21, 2014
NDEGE NNE ZILIWAHI KUPOTEA TANZANIA.
Do you like this story?
Wakati tukio la kupotea kwa ndege ya Shirika
la Ndege la Malaysia, MH370, linaendelea kuitikisa dunia, imebainika kuwa
Tanzania si jambo jipya kutokana na kuwapo kwa kumbukumbu ya matukio manne
tofauti kama hayo katika miongo minane iliyopita.
Ndege hiyo ya Malaysia ilipotea wiki mbili
zilizopita ikiwa na abiria 227 na wafanyakazi 12 huku juhudi za kuitafuta
zinazofanywa na nchi 26 zenye uwezo mkubwa wa kiuchunguzi zikiwa hazijazaa
matunda.
Kwa matukio ya Tanzania, Mkaguzi Mkuu wa
Ajali za Ndege kutoka Wizara ya Uchukuzi, John Nyamwihura amesema katika
mahojiano maalumu na mwandishi wetu kuwa Tanzania imewahi kuingia katika
kumbukumbu za ndege ndogo kupotea na baadhi hazikuonekana kabisa na nyingine
zilionekana baada ya miaka kadhaa kupita. Ndege ya kwanza kupotea ilikuwa mwaka
1937 iliyokuwa ikitoka Tanzania kwenda Madagascar. Ilikuwa na abiria wanane na
haijaonekana hadi leo.
Mbali na tukio hilo ambalo limedumu kwa miaka
77 sasa, Nyamwihura alisema tukio la pili ni la mwaka 2003 wakati ndege
iliyokuwa ikitoka Tanzania kwenda Zambia ilipopotea ikiwa na raia wawili wa
Afrika Kusini, nayo pia haijaonekana hadi sasa.
Mkaguzi huyo alisema katika matukio mengine
mawili, ndege zilizopotea zilionekana baadaye. Mwaka 1997, ndege ndogo
iliyokuwa na abiria mmoja ilipotea katika bonde kwenye kilele cha Kibo, Mlima
Kilimanjaro baada ya kutumbukia kwenye korongo na kuganda kwenye barafu bila
kuonekana hadi baada ya miaka sita. Hata ilipoonekana haikuwezekana kutolewa.
“Ndege ile ilikuwa ikitoka Nairobi kwenda
Zanzibar ikiwa na rubani wa Kitanzania peke yake,” alisema Nyamwihura.
Ndege nyingine iliyoingia katika orodha hiyo
ni ile iliyoanguka katika Ziwa Victoria mwaka 1976 ikiwa na abiria 12 ambayo
ilionekana miaka miwili baadaye.
Nyamwihura akisema sababu kubwa ya matukio
hayo ni mabadiliko ya hali ya hewa na kuharibika kwa miundombinu, mambo ambayo
husababisha kukatika kwa mawasiliano kati ya waongoza ndege na marubani.
“Matukio mengi kama haya ni kuwa ndege
hugonga milima na kuanguka. Zikianguka sehemu za milima ni vigumu kupatikana
kwa sababu wakati mwingine huganda katika barafu au kuzama kwenye makorongo,”
alisema.
Alisema hata ndege zinazoanguka kwenye maji,
pia ni vigumu kuonekana kutokana na kina kirefu au barafu.
Mtaalamu huyo alisema kuna baadhi ya ndege
ambazo hupotea kutokana na rubani kukata mawasiliano kwa makusudi kwa sababu
ama za kigaidi au magendo.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “NDEGE NNE ZILIWAHI KUPOTEA TANZANIA.”
Post a Comment