Friday, May 23, 2014
EMMANUEL ANORD OKWI ALAMBA MILIONI 10 KWA SAA YANGA.
Do you like this story?
STRAIKA, Emmanuel Okwi ameichezea Yanga
dakika 687 kwenye mechi nane kwa msimu ulioisha na kuzoa kitita cha Sh120
Milioni sawa Sh 10 Milioni kwa kila saa moja aliyochezea klabu hiyo ya Jangwani
ndani ya jezi namba 25.
Fungu hilo linahusisha mishahara na dau
la usajili. Katika miezi hiyo minne, amefunga mabao matatu tu.
Lakini mabao hayo hayakuwa na madhara
chanya kwa Yanga kwani mawili alifunga Yanga ikiwa imeshinda mabao 7-0 dhidi ya
Ruvu Shooting kwenye Ligi na moja aliifunga Simba iliposhinda mabao 3-1 kwenye
Mtani Jembe.
Mabao ya mchezaji huyo ambaye imeanza
kudaiwa kwamba anafikiria kuvunja mkataba na Yanga kutokana na ushawishi wa
wagombea wa Simba hayakuipa Yanga faida yoyote zaidi ya kuongeza idadi.
Okwi ambaye sasa yupo katika mgogoro na
Yanga akitaka amaliziwe fedha zake za usajili, ameichezea klabu yake mechi hizo
huku akikosa nyingine saba kwa sababu mbalimbali ikiwemo kugoma na kukosa
kibali.
Nyota huyo aliyeanza kibarua chake
Yanga mwishoni mwa mwaka jana baada ya kusaini mkataba wa miaka miwili na nusu,
ameichezea Yanga kwa dakika 687 (Sawa na michezo nane) ambazo ni mechi za Ligi
Kuu Bara na Ligi ya Mabingwa Afrika lakini akaunti yake ikafurika Sh120
Milioni.
Kati ya Sh120 Milioni alizolipwa Okwi,
Sh 96 Milioni alilipwa kama sehemu ya ada yake ya usajili alipojiunga na Yanga
lakini Sh. 24 Milioni alilipwa kama mshahara wake kwa miezi minne aliyocheza
kabla ya kugoma akishinikiza kumaliziwa kulipwa fedha zake za usajili.
Kwa mwezi Okwi analipwa dola 4,000
ambazo ni zaidi ya Sh. 6 Milioni hivyo kwa miezi minne alilipwa Sh. 24 milioni.
Okwi alisajiliwa kwa dau la dola 100,000 ambazo ni zaidi ya Sh. 160 Milioni,
lakini Yanga ilimlipa kianzio cha dola 60,000 (Sh96 Milioni) hivyo sasa anaidai
dola 40,000 zilizobaki.
Mechi alizoichezea Yanga ni sita za
ligi kuu ambazo ni dhidi ya Ruvu Shooting, Mtibwa Sugar, Azam FC, Rhino
Rangers, Prisons (hakucheza dakika zote tisini) na Mgambo JKT, wakati kwa
upande wa michezo ya kimataifa amecheza mechi mbili nyumbani na ugenini dhidi
ya Al Ahly ya Misri kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika.
Kutokana na kibali chake kuchelewa
kuwasili nchini, Okwi alikosa mechi tatu za mwanzo za mzunguko wa pili wa ligi
kuu ambazo ni dhidi ya Ashanti United, Coastal Union na Mbeya City. Mechi
nyingine aliokosa Okwi ni dhidi ya Komorozine de Domoni ya Comoro iliyokuwa ya
Ligi ya Mabingwa Afrika.
Pia straika huyo aligomea michezo ya
mwisho ya ligi hiyo dhidi ya Simba, JKT Oljoro, JKT Ruvu na Kagera Sugar.
Ukiachana na mechi hizo nane za
michuano mbalimbali, Okwi aliichezea Yanga mechi ya kwanza dhidi ya Simba
Desemba mwaka jana mchezo maalumu wa kirafiki uliopewa jina la Nani Mtani
Jembe, pia alicheza mechi nne za kirafiki walipokuwa kambini Uturuki.
Rekodi zinaonesha kuwa tangu Okwi
aondoke Simba mwaka 2012, amecheza jumla ya michezo 14 tu za kimichuano kwenye
nchi tatu tofauti za Tunisia, Uganda na Tanzania. Aliichezea mechi mbili Etoile
Du Sahel ya Tunisia, akacheza nne Uganda akiwa na SC Villa na nane akiwa na
Yanga.
Akiwa Tunisia Okwi aliichezea mechi
mbili Sahel akitokea benchi lakini hakuweza kuwa na maisha mazuri kwani
aliachana na timu hiyo na kutimkia Uganda alipocheza mechi nne za Ligi Kuu ya
Uganda baada ya kutokea matatizo ya malipo yake.
Kwa sasa Okwi yupo Uganda huku majaliwa
yake katika kikosi cha Yanga yakiwa shakani kwani mwenyewe anadai amaliziwe
fedha zake za usajili lakini uongozi unamtaka ajieleze kwa nini amegoma
kuichezea timu hivyo unapanga kumkata sehemu ya fedha zake za usajili.
Mwenyekiti wa Yanga, Yusuf Manji
(pichani) amesisitiza kwamba kwavile mchezaji huyo haikutumikia Yanga ipasavyo
lazima wakae mezani wajadiliane mambo mawili aongeze mkataba mpaka kufikia
miaka mitatu au wamkate kiasi cha fedha anazoidai.
Lakini mwanasheria wake, Edgar Aggaba
amejibu kwamba hakuna kitu kama hicho, Manji anapaswa kulipa dau
walilokubaliana halafu wakae mezani wazungumze mengine.
Chanzo: Mwanaspoti
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “EMMANUEL ANORD OKWI ALAMBA MILIONI 10 KWA SAA YANGA.”
Post a Comment