Tuesday, June 3, 2014

POLISI WANOLEWA UCHAGUZI MKUU WA 2015



. Harakati za kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2015 zimeanza. Polisi wameanza mafunzo yatakayowaongezea uwezo wa kusimamia uchaguzi huo.

Mafunzo hayo yanafadhiliwa na Shirika la Mpango wa Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), kupitia mradi wake wa Uwezeshaji wa Demokrasia (DEP).

Wakufunzi wanane kutoka Chuo cha Polisi cha Uingereza wanaendesha mafunzo kwa maofisa 88 wa polisi wa ngazi za juu na kati.

Akizungumza katika ufunguzi wa mafunzo hayo, Naibu Kamishna wa Polisi, Simon Sirro amesema yamekuja wakati mwafaka wakati jeshi hilo likijiandaa kwa shughuli hiyo muhimu ya kitaifa.
Mafunzo hayo yanayofanyika Dar es Salaam na Zanzibar yanalenga kuwajengea uwezo makamanda wa polisi wa kupanga, kumudu na kuratibu kwa ufanisi hatua za kipolisi za matukio yanayotishia utulivu wa amani katika jamii.

Amesema katika kila kozi ambayo itaendeshwa kwa wiki mbili, itatoa mafunzo kwa maofisa hao ya kuheshimu haki za binadamu, utawala wa sheria na namna ya kudhibiti ghasia na baadaye kuwafundisha askari wote waliobaki. “Tunataka maofisa wetu wawe na ujuzi wa kutosha kusimamia wakati wa vurugu ili uchaguzi ujao uwe wa haki na amani. Wawe na uwezo mzuri wa kuwaelewesha wananchi juu ya kazi yao ili kuendeleza imani juu ya polisi nyakati kama hizo. Pia yatatusaidia kutambua namna gani tufanye kazi katika mazingira ya vurugu yenye watoto na wanawake.”

Alipoulizwa juu ya matumizi ya nguvu nyingi kwa raia, Sirro alisema wasingependa polisi kutumia nguvu hizo lakini mazingira husika hulazimisha hali hiyo kutokea.

Mtaalamu wa masuala ya usimamizi wa uchaguzi wa UNDP nchini, William Hogan alisema taasisi yake inathamini uchaguzi mkuu, pia namna polisi wanavyotumika katika uchaguzi katika nchi za kidemokrasia. “Umakini wa polisi wakati wa usimamizi wa uchaguzi hususan katika kuheshimu haki za binadamu na utawala wa sheria ni moja ya vitu muhimu ambavyo hupima iwapo uchaguzi husika ulikuwa wa haki na wazi hivyo polisi wanahitajika kuongezewa uwezo,” amesema Hogan.
\
Amesema mafunzo hayo ni mwendelezo tu wa mafunzo kwa polisi kwani yalishafanyika 2010 na yalikuwa na mafanikio.
Amesema wanataka uchaguzi mkuu ujao uwe bora ulimwenguni kwa kuanzia na kuheshimu haki za binadamu na utawala wa sheria.

0 Responses to “POLISI WANOLEWA UCHAGUZI MKUU WA 2015”

Post a Comment

More to Read