Thursday, October 15, 2015
RAIS KIKWETE ASEMA WEWE UPO NJE YA KITUO, UTALINDAJE KURA.
Do you like this story?
RAIS Jakaya Kikwete ametangaza vita na wapigakura
watakaobakia maeneo ya vituo vya uchaguzi baada ya kupigakura zao, akisema
watakuwa wanavunja sheria za nchi.
Akiwa ni Amiri Jeshi Mkuuu wa majeshi ya ulinzi na usalama, Rais
Kikwete ameonya kwamba watakaokaa vituoni ‘watashughulikiwa’ na serikali.
Ametoa tamko hilo mchana leo alipokuwa akihutubia kilele cha
mbio za mwenge wa uhuru kwenye Uwanja wa Jamhuri, mjini Dodoma. Hafla hiyo
ilihudhuriwa pia na Waziri wa Habari, Vijana na Michezo, Dk. Fenella Mukangara
pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Chiku Galawa.
Rais ambaye dhahiri ametoa majibu ya kilichojitokeza kuwa ni
malumbano yanayoendelea kati ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jeshi la
Polisi na Serikali kwa upande mmoja na kwa upande wa wili viongozi wa vyama vya
siasa vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA).
Wakati Tume na serikali wamekuwa wakisisitiza kuwa wananchi
hawatakiwi kukaa maeneo ya karibu na vituo vya uchaguzi baada ya kupiga kura,
viongozi wa UKAWA – Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi na NLD – wanahimiza watu kubakia
vituoni masafa ya mita 100 nje ya vituo kwa ajili ya kujiandaa kulinda kura za
wagombea wao.
Oktoba mosi mbele ya umati mkubwa wa wananchi kwenye viwanja
vya Tanganyika Packers, Kawe, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alisema,
“mkishapiga kura, wanawake nendeni nyumbani, wanaume mtakaa umbali wa mita 200
unaotakiwa kisheria na mtakaa hapo mkilinda kura zenu mpaka matokeo
yatakapopatikana.”
Viongozi wa UKAWA wanasema kwamba hakuna haki kwa wananchi
kuambiwa waende kusubiri matokeo ya uchaguzi majumbani kwao wakati kuna dalili
nyingi za kutokuwepo uhakika kuwa Tume itamudu kuzilinda kura dhidi ya
kuchakachuliwa.
Tume ya Uchaguzi imekuwa ikijitahidi kuonesha uwazi katika
mifumo ya ushughulikiaji kura ingawa imekataa katakata kuonesha mifumo ya
ujumlishaji wa kura wakati daftari lenyewe imelitoa jana kwa ajili ya
kuhakikiwa na vyama vinavyoshiriki uchaguzi.
Katika hali hiyo ya malumbano, Rais Kikwete anajitokeza
kusema kuwa serikali haitamvumilia mtu yeyote anayekusudia kuvunja sheria
kipindi cha uchaguzi kwa kuwa hayuko tayari kuona demokrasia “inatekwa nyara.”
Rais analalamika kwa kuhoji, “Mnakaa nje ya vituo vya
kupigia kura kufanya nini? Wewe upo nje ya kituo, utalindaje kura? Mtu wa
kulinda kura ni wakala wa chama chako, labda kama ni mzembe.”
“Mipango ya kuvuruga amani inafahamika na itadhibitiwa watu
wao wapige kura mapema na wanawake waende nyumbani, wanaume wabaki kulinda
kura, wanadhani wengine hawawezi kuwahi… msiilazimishe serikali kufanya mambo
yasiyopendeza, wanaotaka kufanya fujo hawatavumiliwa waatadhibitiwa,” amesema.
“Mkishapiga kura nendeni nyumbani Tume ya Uchaguzi
imeshafafanua vizuri suala hili… tofauti na hapo ni vurugu, na sisi kama
serikali hatutawavumilia watakaokiuka sheria. Tutawadhibiti kwa nguvu ileile
watakayoitumia,” amesema katika hotuba iliyotangazwa moja kwa moja na vituo vya
televisheni.
Rais Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM Taifa amedai
suala la kulinda kura ni mkakati wa viongozi wa vyama vya siasa kuwazuia baadhi
ya wananchi kupigakura baada ya wanachama wa vyama vyao kupiga kura.
Huko nyuma, viongozi wa UKAWA walishatangaza kuwa
watayatangaza matokeo ya kura za urais hata kabla ya Tume, kwa kuwa sheria
inaruhusu kutangaza kura zinazokamilika kuhesabiwa na kuidhinishwa na wagombea
na mawalaka wao almuradi sio matokeo ya majimbo yote.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “RAIS KIKWETE ASEMA WEWE UPO NJE YA KITUO, UTALINDAJE KURA.”
Post a Comment