Monday, March 24, 2014
MWANDISHI UINGEREZA AIBUA MAPYA MENO YA TEMBO TANZANIA.
Do you like this story?
Licha ya Rais Jakaya Kikwete kutoa ahadi ya
kuteketeza maelfu ya meno ya tembo yaliyo kwenye ghala la Serikali, imeelezwa
kuwa uwezekano huo ni mdogo.
Mwandishi wa gazeti la Daily Mail la
Uingereza, Martin Fletcher ameeleza kushtushwa na hali ya ulinzi kwenye ghala
hilo lililosheheni meno 34,000 ya tembo ambayo kwa biashara ya magendo nchini
China yanagharimu Pauni 150 milioni za Kiingereza (Sh403.5 bilioni)
Fletcher, ambaye aliandika habari ya kuhusika
kwa wanasiasa na wafanyabiashara wakubwa wa Tanzania katika biashara haramu ya
meno hayo kiasi cha kuifanya nchi kuwa muuzaji mkuu wa nyara hizo, aliandika
hayo kwenye taarifa kuhusu ziara yake nchini iliyochapishwa na gazeti hilo
jana.
Habari ya awali ilitikisa ulimwengu ambao
unapambana kulinda viumbe walio hatarini kutoweka ikiwatuhumu wanasiasa na
wafanyabiashara wakubwa nchini kuhusika, huku Serikali ikishindwa kuwadhibiti.
Habari hiyo iliifanya Serikali ya Tanzania
kufungua milango kwa vyombo vya habari vya nje kuja nchini kupata habari sahihi
kuhusu tatizo hilo, akiwamo Fletcher wa Daily Mail.
Katika ziara yake, Fletcher alipata nafasi ya
kutembelea ghala la nyara hizo, kuzungumza na maofisa wanyama pori pamoja na
Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu.
“Nyalandu pia aliweka bayana kuwa uteketezaji
wa shehena ya Tanzania ni kitu ambacho kiko mbali na uhalisia, licha ya ahadi
ya Kikwete jijini London,” Fletcher alimkariri Nyalandu kwenye habari hiyo
ambayo imeambatana na picha alizozielezea kuwa za kushtua za ghala hilo, lenye
idadi kubwa ya meno ya tembo kuliko maghala yote duniani.
“Amesema Rais alikuwa na nia ya kuteketeza
(shehena hiyo), lakini Tanzania ilitaka ilipwe takriban Pauni 30 milioni za
Uingereza kutoka Jumuiya ya Kimataifa kwa ajili ya Mfuko wa Hifadhi ya Tembo.”
Hata hivyo mwandishi huyo anaripoti kuwa;
“Wahisani ambao wangeweza kutoa fedha hizo, walikejeli kiwango hicho wakisema
hakina uhalisia.”
Alipoulizwa kuhusu kauli hiyo jana, Nyalandu
alisema baadhi ya mambo kwenye habari ya mwandishi huyo yamekuzwa, lakini
alisema uamuzi wa kuteketeza nyara hizo haujafikiwa.
Amesema Serikali ilichofanya hadi sasa ni
kupiga marufuku biashara zote za meno ya tembo, hivyo haitauza yaliyopo na
haitaomba kibali tena cha kufanya biashara hiyo na kwamba kinachoendelea sasa
ni mazungumzo ya namna ya kushughulika na shehena iliyopo.
“Meno mengine yaliyopo ni ya kihistoria. Ni
marefu kuliko mengine na tembo wa aina hii hawapo tena, hivyo kuwa nayo pia ni
kitu kizuri. Haya meno ni mali ya Watanzania wote, uamuzi wa kuyateketeza
lazima uchukuliwe kwa busara,” alisema.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “MWANDISHI UINGEREZA AIBUA MAPYA MENO YA TEMBO TANZANIA.”
Post a Comment