Friday, September 26, 2014
UDA YAWAFUKUZA KAZI MADEREVA 12
Do you like this story?
SHIRIKA la Usafiri
Dar es Salaam (UDA) limewafukuza kazi madereva wake 42 kwa makosa mbalimbali,
yakiwemo utovu wa nidhamu.
Makosa mengine
yaliyosababisha wafukuzwe kazi ni, kuvunja sheria za barabarani kwa makusudi,
kukatisha njia kinyume cha taratibu na kutoza nauli zisizo rasmi tofauti na
zilizopo kwenye tiketi.
Akizungumza na
waandishi wa habari jana Dar es Salaam, Msemaji wa Uda, George Maziku alisema
wamefukuzwa kutoka vituo vya kazi vya shirika ambavyo ni Gongo la Mboto,
Mbagala, Kamata na Boko 2.
Alisema shirika
limefikia uamuzi huo baada ya kuridhishwa na matokeo ya uchunguzi uliofanywa na
kikosi kazi chake cha kufuatilia mwenendo wa madereva wawapo barabarani.
Alitaja makosa
mengine ni kufanya kazi wakiwa wamelewa, kutoa lugha chafu kwa askari wa
usalama barabarani na kwa abiria pamoja na kukithiri kwa uchafu.
“Sisi tumewafukuza
kazi kutokana na makosa ambayo nimeyasema hapo mwanzo, UDA hatuwezi kuvumilia
watu wa namna hii wanaofanya makosa makusudi bila kuzingatia taratibu na kanuni
zilizopo za usafiri usafiri wa umma,” alisema Maziku.
Kwa mujibu wa Maziku,
lengo la Uda ni kuboresha sekta ya usafiri wa umma katika jiji la Dar es Salaam
na kuwaondolea wateja kadhia.
Aidha alisema shirika
limekuwa likichafuliwa na madereva wazembe wenye tabia mbovu kiutendaji,
wanaoonesha sifa mbaya kwa jamii.
Wakati huo huo, Jeshi
la Polisi mkoa wa kipolisi wa Ilala jijini Dar es Salaam, kwa kushirikiana na
mkufunzi wa chuo cha udereva cha Lumumba, Tilya Condrad wametoa mafunzo ya
usalama barabarani kwa madereva 40 wa UDA.
Mafunzo hayo
yalitolewa jana ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Wiki ya Nenda kwa Usalama
Barabarani.
Mkufunzi huyo
alipongeza shirika kwa kujali abiria wake kwa kutilia uzito mafunzo ya usalama
barabarani kwa madereva wao.
Wakizungumza kwa
nyakati tofauti madereva hao walisema kuwa ni mpango mzuri unaofanywa
kuwajengea ufahamu juu ya umuhimu wa usalama barabarani.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “UDA YAWAFUKUZA KAZI MADEREVA 12 ”
Post a Comment