Friday, March 28, 2014
SAMWELI SITTA AWEKWA MTEGONI.
Do you like this story?
Suala la ama kutumia kura ya siri au ya wazi
kuamua ibara za Rasimu ya Katiba jana liliuteka upya mjadala wa Kanuni za Bunge
la Katiba, huku ikielezwa kuwa limewekwa kama mtego kwa Mwenyekiti wa Bunge
hilo, Samuel Sitta katika kuwania urais.
Sitta ni mmoja wa wanasiasa wanaotajwa kuwa
katika kinyang’anyiro cha urais katika uchaguzi mkuu ujao kupitia CCM, huku
akikabiliwa na upinzani mkali kutoka kwa mahasimu wake kisiasa ndani ya chama
hicho.
Mjumbe wa Bunge la Katiba, Godbless Lema
alimtaka Sitta kuwa makini na maelekezo aliyodai mwenyekiti huyo anapewa katika
uendeshaji wa Bunge na kudai pia kuwa, kuna kundi la watu wanaotaka urais
katika Uchaguzi Mkuu 2015 wanaotaka kumkwamisha.
Akichangia hoja ya mapendekezo ya mabadiliko
ya kanuni yaliyotaka kupitishwa mifumo miwili ya kura kwa wazi na siri, Lema
ambaye ni Mbunge wa Arusha alisema kwa mazingira ambayo yanaendelea, Sitta
anapaswa kuwa makini na watu wanaompatia maelekezo wakitaka aonekane hafai
baadaye.
“Ni vyema ukawa makini na mapendekezo
unayoletewa kwa sababu hao wote pamoja na wanachama wa chama chako wanajua kama
utaliongoza vizuri Bunge hili, basi unaweza ukapata tiketi ya kugombea urais
2015 ndani ya chama chako, lakini ukishindwa watakudhihaki kuwa umeshindwa,
hivyo hutaweza kuliongoza taifa,” alisema Lema huku Sitta aliyeonekana awali
akitabasamu, alibadilika na kumtazama mbunge huyo kwa umakini.
Lema alisema miongoni mwa wajumbe wa Kamati
Kuu ya CCM na kamati nyingine za Bunge hilo, kuna watu ambao wanataka kugombea
urais katika uchaguzi mkuu ujao.
Katika mjadala huo, ilionekana wazi kuwa
wajumbe bado wamegawanyika pande mbili – CCM wakionekana kuunga mkono kura ya
wazi na upande wa upinzani wakipigia chapuo kura ya siri.
Miongoni mwa waliopigia debe kura ya siri ni
John Mnyika aliyesema suala la upigaji kura ni la kikatiba ili kuhakikisha kila
mjumbe anapiga kura yake bila kushurutishwa, kushinikizwa wala kupokea
maelekezo kutoka kwa mtu au chombo chochote.
Wajumbe hao walikuwa wanajadili mapendekezo
yaliyowasilishwa jana na Mwenyekiti wa Kamati ya Kanuni na Haki za Bunge, Pandu
Ameir Kificho, baada ya juzi kuzua mvutano uliosababisha Bunge hilo kuvunjika
ili kusubiri maridhiano ya pande zinazopingana.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “SAMWELI SITTA AWEKWA MTEGONI.”
Post a Comment